• HABARI MPYA

    Monday, August 27, 2018

    YANGA SC KUIFUATA RAYON BILA MAKAPU, AMEFIWA NA MAMA YAKE MZAZI MAZISHI LEO ZANZIBAR

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KIUNGO wa Yanga SC, Said Juma ‘Makapu’ hatasafiri na timu kwenda Kigali nchini Rwanda kwa ajili ya mchezo wa mwisho wa Kundi D Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Rayon Sport, kufuatia kufiwa na mama yake mzazi nyumbani kwao Zanzibar.
    Taarifa ya Yanga SC jana imesema kwamba mama yake Makapu amefariki dunia jana asubuhi huko Bububu visiwani Zanzibar na mazishi yanatarajiwa kufanyika leo baada ya sala ya Adhuhuri.
    Kikosi cha Yanga kinatarajiwa kuondoka Dar es Salaam leo usiku kwenda Kigali kwa ajili ya mchezo huo wa mwisho baada ya kushinda mechi moja tu kati ya tano za awali, kufungwa tatu na sare moja.

    Said Juma 'Makapu' (kushoto) amefiwa na mama yake mzazi nyumbani kwao, Zanzibar

    Mchezo huo utakaofanyika Jumatano kuanzia Saa 9:00 Alasiri Uwanja wa Nyamirambo, utachezeshwa na marefa kutoka Uganda, Mashood Ssali atakayepuliza filimbi akisaidiwa na washika vibendera Mark Ssonko na Dick Okello. 
    Mchezo wa kwanza baina ya Yanga na Rayon Sport, wote mabingwa wa zamani wa Afrika Mashariki na Kati timu hizo zilimaliza kwa sare ya 0-0 Mei 16 Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam.
    Yanga SC inashika mkia katika kundi D, ikiwa na pointi nne tu, nyuma ya Rayon yenye pointi sita, wakati Gor Mahia na USM Alger kila moja ina pointi nane na zinamenyana kwenye mechi ya mwisho Jumatano pia mjini Algiers.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC KUIFUATA RAYON BILA MAKAPU, AMEFIWA NA MAMA YAKE MZAZI MAZISHI LEO ZANZIBAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top