• HABARI MPYA

    Thursday, August 30, 2018

    RONALDO USO KWA USO NA MOURINHO MAN UNITED

    MWANASOKA bora wa dunia, Cristiano Ronaldo atarejea Old Trafford baada ya Manchester United kupangwa Kundi H pamoja na mabingwa wa Italia, Juventus.
    Tottenham ina mtihani mgumu wa kufuzu hatua ya 16 ya Ligi ya Mabingwa Ulaya baada ya kupangwa Kundi B na Barcelona.
    Manchester City wana njia nyepesi ya kwenda hatua ya mtoano kutokana na Shakhtar Donetsk kuwa wapinzani pekee wagumu katika Kundi F. Liverpool watamenyana na Paris Saint-Germain na Napoli katika Kundi C. 
    Mbali na Ronaldo na Juventus yake kuwa wapinzani wagumu, United watatarajia upinzani mwepesi kutoka kwa Valencia na Young Boys, ambao wamerejea kwenye hatua ya makundi mwaka huu.

    Cristiano Ronaldo atakwenda tena Old Trafford kumkabili kocha wake wa zamani, Jose Mourinho wa Manchester United 

    Ronaldo mwenye umri wa miaka 33 anataka kushinda taji la nne mfululizo la Ligi ya Mabingwa baada ya kushinda matatu na Real Madrid misimu mitatu iliyopita.  
    Katika Kundi B, kocha Mauricio Pochettino wa Tottenham atakutana na wapinzani wagumu kwa mara ya pili mfululizo baada ya msimu uliopita kuwafunga Borussia Dortmund na Real Madrid.
    Lakini msimu huu Pochettino amepangwa na Barcelona, ambayo haijawahi kuifunga Tottenham,PSV Eindhoven na Inter Milan.
    Mabingwa wa Ligi Kuu England, City wamevuna matunda ya kazi yao nzuri msimu uliopita wakipangwa na Shakhtar Donetsk, mabingwa wa Ukraine, ambao ndiyo watakuwa wapinzani wagumu zaidi kwenye Kundi F. 

    Kikosi cha Pep Guardiola pia kitamenyana na Lyon na Hoffenheim, wakati watahitaji kurudia soka yao nzuri iliyowafikisha fainali msimu uliopita.
    Katika Kundi C, kikosi cha Jurgen Klopp kitamenyana na PSG, Napoli na Red Star Belgrade.
    Kiungo wa zamani wa Real Madrid, Kaka na mchezaji wa zamani wa Manchester United, Diego Forlan waliongoza droo hiyo leo ukumbi wa Grimaldi Forum mjini Monaco, Ufaransa.
    Raundi ya kwanza ya mechi za makundi itaanza Jumanne ya Septemba 18 na fainali itachezwa Juni 1 nyumbani kwa Atletico Madrid, Uwanja wa Wanda Metropolitano mjini Madrid.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: RONALDO USO KWA USO NA MOURINHO MAN UNITED Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top