• HABARI MPYA

    Thursday, August 30, 2018

    GHARAMA ZA KUWAONDOA WACHEZAJI WA SIMBA TAIFA STARS NI KUBWA KULIKO AJUAVYO KIDAU

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limechukua maamuzi magumu baada ya jana kuamua kuwaondoa wachezaji saba kwenye timu ya taifa, Taifa Stars, sita wa klabu ya Simba SC na mmoja tu wa Yanga kwa kile kilichodaiwa utovu wa nidhamu.
    Hao ni mabeki Shomari Kapombe, Erasto Nyoni, viungo Jonas Mkude, Shiza Kichuya, Hassan Dilunga na mshambuliaji na Nahodha, John Bocco wa Simba SC na kiungo Feisal Salum wa Yanga SC.
    Ikumbukwe Taifa Stars inajiandaa na mechi ya Kundi L kufuzu Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika dhidi ya wenyeji, Uganda maarufu The Cranes, Septemba 8, mwaka huu mjini Kampala.
    Rais anajua? Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli (kulia) akisalimiana na winga wa Simba SC, Shiza Kichuya Mei 19, mwaka huu Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam


    Na Katibu Mkuu wa TFF, Wilfred Kidau alizungumza na Waandishi wa Habari jana mchana akiwa na dalili zote za hasira ndani yake akisema kwamba wachezaji hao walikaidi agizo la kuripoti kambini Taifa Stars licha ya kupigiwa simu.  
    Kidau alisema baada ya wachezaji hao kushindwa kuripoti kambini hoteli ya Sea Scape, eneo la Kunduchi mjini Dar es Salaam bila taarifa yoyote, huku mwenzao, kipa, Aishi Salum Manula pekee akiripoti, kocha mpya Mnigeria, Emmanuel Amunike amewachukulia hatua ya kuwaondoa.
    Kidau amedai Amunike, winga wa zamani wa kimataifa wa Nigeria, amewachukua mabeki, Ally Sonso, Paul Ngalema wa Lipuli FC ya Iringa, Salum Kimenya wa Tanzania Prisons ya Mbeya, David Mwantika, viungo Frank Domayo wa Azam FC, Salum Kihimbwa na mshambuliaji Kelvin Sabato, wote wa Mtibwa Sugar. 
    Wachezaji walioripoti kambini hadi sasa ukiondoa walioongezwa ni makipa Aishi Manula wa Simba SC na Mohammed Abdulrahman Wawesha wa JKU, mabeki ni Aggrey Morris, viungo Mudathir Yahya na mshambuliaji Yahya Zayed wa Azam FC.
    Wachezaji wa Yanga SC, kipa Benno Kakolanya, mabeki Gardiel Michael, Kelvin Yondan na Andrew Vincent ‘Dante’ na kiungo Feisal Salum ambao wapo na timu yao mjini Kigali, Rwanda ambako jana ilikuwa inamenyana na wenyeji, Rayon Sport katika mchezo wa Kombe la Shirikisho Afrika watajiunga na timu wakirejea kuanzia Iiumaa.
    Nyota wanaocheza nje wanatarajiwa kuwasili kuanzia Septemba 1 ambao ni mabeki Hassan Kessy wa Nkana FC ya Zambia, Abdi Banda wa Baroka FC ya Afrika Kusini, Himid Mao wa Petrojet FC ya Misri, Simon Msuva wa Difaa Hassan El-Jadida, Morocco, Farid Mussa, Shaaba Iddi wa CD Tenerife  ya Hispania, Rashid Mandawa wa BDF XI ya Botswana, Emmanuel Ulimwengu wa El HIlal ya Sudan) na Nahodha Mbwana Samatta wa KRC Genk ya Ubelgiji.
    Amunike aliyesaini mkataba wa kufundisha Taifa Stars mapema mwezi huu, ambaye anasaidiwa na Mnigeria mwenzake, Emeka Amadi na Mzalendo, Hemed Suleiman ‘Morocco’, anahitaji ushindi dhidi ya Uganda Septemba 8 ili kufufua matumaini ya kwenda Cameroon mwakani, baada ya  sare ya 1-1 nyumbani na Lesotho Juni 10, mwaka jana Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam ikiwa chini ya kocha mzalendo, Salum Mayanga.
    Mechi tatu za mzunguko wa kwanza, ikiwemo ya Oktoba 10, mwaka huu pia dhidi ya Cape Verde ndizo zinatarajiwa kutoa taswira ya nafasi ya Taifa Stars kwenye kupigania tiketi ya AFCON ya kwanza tangu 1980.
    Bila shaka TFF imemleta Amunike, mchezaji wa zamani wa Barcelona baada ya kujiridhisha inahiataji mwalimu mgeni wa aina hiyo ili kuongeza nguvu ya kiufundi kwenye timu katika jiithada za kusaka matokeo mazuri.
    Amunike anatarajiwa kukutana na wachezaji wa Taifa Stars kwa mara ya kwanza kabisa katika kambi hii baada ya kuajiriwa mapema mwezi huu.

    Wachezaji wazoefu na walio fiti John Bocco (kulia) na Shomari Kapombe (kushoto) wameondolewa

    Na hata kikosi hiki, si uteuzi wake wala Msaidizi wake, Emeka Amadi labda asingiziwe Msaidizi namba mbili, mzalendo Hemed Suleiman ‘Morocco’. Lakini hata walioteua hawajakosea sana, kwa sababu idadi kubwa ni wachezaji waliokuwemo kwenye kikosi cha kocha aliyeondolewa, Mayanga.
    Katika kambi yake hii ya kwanza ya Taifa Stars, kocha Emmanuel Amunike alihitaji kukutana na wachezaji wote nyota wa Tanzania ambao hata TFF wanaamini ndiyo wanastahili kuchezea timu ya taifa kwa sasa ili awafahamu vizuri.
    Kulikuwa kuna haja haswa ya TFF kuhakikisha Amunike anakutana na wachezaji wote nyota wanaoonekana wanafaa kwa Taifa Stars, awaone na kuwajua vizuri kwa nadharia na vitendo.
    Lakini ajabu TFF imejiruhusu kuingia katika mgogoro usio wa lazima na wachezaji wengine nyota, jambo ambalo linamnyima fursa sasa kocha Amunike kukutana na wachezaji wote nyota wa nchi.
    Hata kama kambi ya Taifa Stars ingeanza Septemba 1 bado ni muda mzuri wa kutosha wa maandalizi kwa wachezaji ambao wanatoka kwenye klabu zao wakiwa wanacheza. Lakini, kungekuwa na ubaya gani wachezaji walioondolewa kikosini wangepewa nafasi hadi leo baada ya kushindwa kuripoti jana?
    Katibu wa TFF, Kidau kwa umri wake anaweza kugombea hata Urais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania – hivyo ni mtu aliyekomaa hapana shaka na kwa elimu yake ya wastani ya darasani, kucheza soka hadi klabu kubwa ya Simba na timu ya taifa hizo ni sifa tosha za kuwa kiongozi wa nafasi yake.

    Rais wa TFF, Wallace Karia (kulia) anatakiwa kumpunguzia nguvu ya maamuzi Katibu Mkuu wake, Wilfred Kidau ambaye anaonekana ni mwenye jazba

    Lakini kuna kitu Kidau anakosa na wasiwasi ni kwamba katika umri huu ni vigumu mno kumbadili, zaidi tu kumdhibiti. Baada ya kumfuatilia kwa muda wa kutosha, inatosha kusema Kidau hana subira na ni mtu mwenye maamuzi ya jazba, tena ambaye ‘anapopandisha’ hakuna anayeweza kumzuia.
    Watu wa aina hii ukiwapa majukumu mazito kama aliyopewa Kidau, lazima uwadhibiti wasiwe na maamuzi ya mwisho.  Gharama za kuwaondoa wachezaji hao saba kikosini Taifa Stars ni kubwa kuliko kuwavumilia kwa saa 48 – ukiwa na jazba huwezi kulijua hilo. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: GHARAMA ZA KUWAONDOA WACHEZAJI WA SIMBA TAIFA STARS NI KUBWA KULIKO AJUAVYO KIDAU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top