• HABARI MPYA

    Sunday, March 18, 2018

    NGORONGORO HEROES YAIBAMIZA MOROCCO 1-0 UHURU MBELE YA WAZIRI MKUU MAJALIWA

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    TIMU ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 20, Ngorongoro Heroes imepata ushindi mwembamba wa 1-0 dhidi ya Morocco katika mchezo wa kirafiki uliofanyika Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam jioni ya leo.
    Katika mechi hiyo iliyohudhuriwa na Waziri Mkuu, Dk. Kassim Majaliwa, bao pekee la Tanzania limefungwa na Muhsin Makame aliyetokea benchi kipindi cha pili.
    Makame mmoja kati ya wachezaji wengi wanaounda Ngorongoro waliokuwa timu ya vijana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys iliyoshiriki fainali za Afrika nchini Gabon Mei mwaka jana, alifunga bao hilo kwa penalti dakika ya 62.
    Muhsin Makame akishangilia baada ya kuifungia bao pekee Ngorongoro Heroes leo 
    Beki wa Morocco, Bah Said Nolad (kulia) akimdhibiti mshambuliaji wa Tanzania, Amani Maziku
    Kiungo wa Tanzania, Said Mussa 'Ronaldo' akijivuta kumpita Bousbaa Idriss wa Morocco  
    Kiungop wa Tanzania, Assad Juma akiwatoka wachezaji wa Morocco 
    Limourt Youssef wa Morocco akimiliki mpira mbele ya Kibwana Shomari wa Ngorongoro

    Na penalti hiyo ilitolewa na refa Mkenya, Anthony Juma Ogwayo baada ya beki wa Morocco na nahodha Bah Said Nolad kuunawa mpira uliopigwa Assad Ali Juma.
    Serengeti Boys iliyo chini ya kocha Ammy Ninje anayesaidiwa na jopo, Juma Mgunda, Leopold Tasso, Manyika Peter na Boniface Pawasa ilicheza vizuri na kutengeneza nafasi nyingi za kufunga hususan kipindi cha pili, lakini umaliziaji mbovu ukawakosesha mabao zaidi.
    Serengeti Boys itateremka tena dimbani Jumatano kumenyana na Msumbiji katika mchezo mwingine wa kirafiki, kabla ya kucheza na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) katika mechi ya kwanza ya kuwania tiketi ya Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON U20) Machi 31.
    Kesho kutakuwa na mchezo mwingine wa kirafiki baina ya wageni watupu, Morocco na Msumbiji Uwanja wa Uhuru pia ambao pia mashabiki wataingia bure kama ilivyokuwa leo.
    Tanzania; Aboutalib Msheri, Kibwana Shomari, Nickson Kibabage, Ally Msengi, Dickson Job, Ally Ng’anzi, Assad Juma, Kelvin Naftali/Shaaban Ada dk79, Amani Maziku/Muhsin Makame dk60, Abdul Suleiman na Said Mussa ‘Ronaldo’/Mohammed Mussa dk60.
    Morocco; Laafsa Zyad, Lanine Yassine, Louzif Nourad/Yakiry Chadi dk46, Bousbaa Idriss, Elovauabi Hatin/Belkhyartou Ssama dk62, Bah Said Nolad, Gareh Oussana/Bachkou Athmane dk75, Limourt Youssef, Rhazooat Abderrazak/Ait Mohamed Karim dk46, Sellak Azzedine/Benchaovi Anovar dk72na Abissi Abdesamad/Joutarajji Israil dk62.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NGORONGORO HEROES YAIBAMIZA MOROCCO 1-0 UHURU MBELE YA WAZIRI MKUU MAJALIWA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top