• HABARI MPYA

    Tuesday, March 20, 2018

    DONALD NGOMA SASA YUKO FITI KABISA KUANZA KUITUMIKIA YANGA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    HII ni habari njema kwa mashabiki wa Yanga, kwa kurejea mshambuliaji wao, Donald Ngoma anatakayeungana na kikosi cha timu hiyo kesho kutwa ndani ya kikosi cha timu hiyo kujiandaa na mchezo wao wa Azam Sports Federation Cup (ASFC) dhidi ya Singida United.
    Ngoma alipata majeraha ya goti katika mchezo wa Ligi Kuu ya Bara dhidi ya Mtibwa Sugar mchezo uliopigwa Septemba 30, mwaka jana ambayo yamemuweka nje ya uwanja kwa miezi sita.
    Akizungumza na Bin Zubeiry Sports – Online leo, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Yanga, Hussein Nyika amesema kwamba kwa mujibu wa taarifa za daktari wa timu hiyo nyota huyo yupo fiti kuanza mazoezi.
    Donald Ngoma sasa anatarajiwa kuanza mazoezi Yanga baada ya kuwa nje tangu Septemba mwaka jana

    “Ngoma tayari amepona ataungana na timu Alhamisi  baada ya kutoka katika majeruhi ya muda mrefu, suala la kucheza au kutokucheza lipo mikononi mwa benchi la ufundi ambalo litaangalia kama amekuwa tayari kuanza kutumika,” alisema Nyika.
    Alisema wachezaji wote waliokuwa majeruhi wamepona na kuungana na kikosi cha timu hiyo kwa ajili ya kujiandaa na mchezo huo wa kombe la ASFC, mchezo wao katika hatua ya makundi ya michuano ya kombe la Shirikisho (CAF).
    Yanga imeondolewa katika Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya sare ya 0-0 na wenyeji, Township Rollers Jumamosi jioni Uwanja wa Taifa mjini Gaborone nchini Botswana.
    Matokeo hayo yanamaanisha Rollers inakwenda hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa kwa mara ya kwanza historia hiyo kwa ushindi wa jumla wa 2-1 uliotokana na matokeo ya mchezo wa kwanza Dar es Salaam Machi 6.
    Yanga itamenyana na moja ya timu zilizofuzu hatua ya 16 Bora ya michuano hiyo, ambazo ni CR Belouizdad, USM Alger za Algeria, Al-Masry ya Misri, Djoliba ya Mali, Raja Casablanca, Enyimba ya Nigeria, SuperSport United ya Afrika Kusini na Al-Hilal Al-Ubayyid ya Sudan.
    Pamoja na Yanga, wapinzani wengine wa timu hizo ni AS Vita ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), ASEC Mimosas, Williamsville AC za Ivory Coast, Saint George ya Ethiopia, CF Mounana ya Gabon, Aduana Stars ya Ghana, Gor Mahia ya Kenya na UD Songo ya Msumbiji.
    Wengine ni MFM, Plateau United za Nigeria, Rayon Sports ya Rwanda, Generation Foot ya Senegal, Bidvest Wits ya Afrika Kusini, Al-Hilal ya Sudan na Zanaco ya Zambia.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: DONALD NGOMA SASA YUKO FITI KABISA KUANZA KUITUMIKIA YANGA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top