• HABARI MPYA

    Sunday, September 23, 2012

    MALINDI YABANWA ZANZIBAR


    Na Ally Mohamed, Zanziabr
    MABINGWA wa zamani wa Zanzibar, Malindi jioni hii wamelazimishwa sare ya kufungana mabao 2-2 na Mafunzo katika mfululizo wa Ligi Kuu ya Zanzibar kwenye Uwanja wa Amaan, Zanziabr.
    Malindi walikuwa wa kwanza kupata bao katika dakika ya 30 likifungwa na Amour Suleiman, ambalo lilidumu hadi dakika 45 za kipindi cha kwanza, kabla ya Mafunzo kusawazisha dakika ya 72 kupitia kwa Ali Juma.
    Katika dakika ya 88, Renatus Morris aliipatia Malindi bao la pili na wakati watazamaji wakiamini Malindi wataondoka na pointi tatu, Jaku Juma alizima ndoto za Malindi baada ya kuifungia Mafunzo bao la kusawazisha dakika ya 89.
    Kisiwani Pemba, mchezo uliochezwa katika Uwanja wa Gombani, Pemba Chipukizi waliifunga Duma, inayomilikiwa na Jeshi la Kujenga Uchumi (JKU) mabao 2-1.
    Mabao ya Chipukizi yalifungwa na Faki Mwalim na Abdulkarim Ali, wakati bao pekee la Duma likifungwa na Maulid Ramadhan.
    Ligi hiyo itaendelea tena kesho kwa mchezo mmoja katika uwanja wa Amaan kisiwani Unguja kwa Mtende Rangers ambaom wamepanda daraja msimu huu kucheza na Mundu.
    Katika mechi za jana, mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Zanzibar, Super Falcon waliendelea kuboronga katika ligi hiyo licha ya kumtimua kocha wake wiki iliyopita, baada ya kuchapwa mabao 2-0 na Jamhuri ya Pemba, kwenye Uwanja wa Gombani, Pemba, wakati Bandari imeibuka na ushindi wa 2-1 dhidi ya KMKM Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
    Uwanja wa Gombani, Falcon ambao wataiwakilisha Zanzibar katika Ligi ya Mabingwa Afrika mwakani, walikubali kipigo cha tatu mfululizo katika ligi hiyo kwa mabao ya Mfaume Shaaban na Abdallah Mohammed, hiyo ikiwa mechi ya nane kwa Super Falcon kupoteza.
    Bandari iliyopanda Ligi Kuu msimu huu ilipata bao lake la kwanza dakika ya 37, lililotiwa kimiani na Mussa Omar, kabla ya KMKM kusawazisha dakika ya 44, mfungaji Mudrik Muhib na Bandari wakapata bao la ushindi dakika 76 kupitia kwa Mohammed Abdallah.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MALINDI YABANWA ZANZIBAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top