• HABARI MPYA

    Saturday, August 18, 2018

    NI SIMBA SC WASHINDI WA NGAO YA JAMII TENA, WAICHAPA MTIBWA SUGAR 2-1 KIRUMBA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    SIMBA SC wamefanikiwa kutwaa Ngao ya Jamii kwa mara ya pili mfululizo baada ya ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Mtibwa Sugar Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza.
    Hiyo inakuwa mara ya nne kwa SImba SC kutwaa Ngao ya Jamii, baada ya 2011 wakiifunga Yanga 2-0, 2012 wakiifunga Azam FC 3-2 na mwaka jana wakiwafunga tena mahasimu wao wa jadi, kwa penalti 5-4 baada ya sare ya 0-0.
    Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa bora wa Ligi Kuu msimu uliopita, Elly Sasii aliyesaidiwa na Hellen Mduma wote wa Dar es Salaam, na Ferdinand Chacha wa Mwanza, hadi mapumziko Simba SC walikuwa mbele kwa mabao 2-1.

    Hassan Dilunga akinyoosha mikono kuwaomba radhi Mtibwa Sugar baada ya kufunga bao la ushindi leo CCM Kirumba

    Mshambuliaji Mnyarwanda mwenye asili ya Uganda, Meddie Kagere alianza kuifungia Simba SC dakika ya 29 kwa shuti kali kutokea pembezoni mwa Uwanja kushoto, baada ya kuwatoka mabeki wa Mtibwa Sugar na kipa wao, Benedictor Tinocco kufuatia kazi nzuri ya Hassan Dilunga.
    Kelvin Sabato Kongwe au Kiduku akaisawazishia Mtibwa Sugar dakika ya 33 baada kupokea pasi nzuri ya Saleh Hamisi na kufumua shuti zuri akiwa anatazamwa na mabeki wa Simba SC.
    Wakati refa Sasii anajiandaa kupuliza filimbi ya kukamilisha kipindi cha kwanza, Hassan Dilunga akaifungia Simba SC bao la pili dakika ya tatu ya muda wa nyongeza baada ya dakika 45 stahili za mchezo.
    Dilunga aliyesajiliwa kutoka Mtibwa Sugar mwezi uliopita tu baada ya awali kuchezea Ruvu Shooting, Yanga SC na JKT Ruvu, alifunga bao hilo kwa shuti lililowababatiza wachezaji wengine kufuatia pasi ya Mganda, Emmanuel Okwi.
    Kipindi cha pili mchezo uliendelea kupendeza, Simba SC wakisaka mabao zaidi na Mtibwa Sugar wakitafuta bao la kusawazisha lakini hakuna timu iliyofanikiwa kutikisa nyavu. 
    Mtibwa ilipata pigo baada ya kiungo wake, Awadh Juma kuumia na kushindwa kuendelea na mchezo, nafasi yake imechukuliwa na Juma Luizio dakika ya 63, wote wamewahi kuchezea SImba SC.
    Nahodha wa leo wa Simba SC, Emmanuel Okwi naye akashindwa kuendelea na mchezo dakika ya 66 akimpisha Nahodha wa klabu, John Bocco. 
    Kikosi cha Simba SC kilikuwa; Aishi Manula, Nicolas Gyan, Asante Kwasi, Erasto Nyoni, Pascal Wawa, Jonas Mkude, James Kotei, Hassan Dilunga/Muzamil Yassin dk78, Meddie Kagere, Emmanuel Okwi/John Bocco dk66 na Shiza Kichuya/Shomari Kapombe dk73.
    Mtibwa Sugar: Benedict Tinoco, Rogers Gabriel, Issa Rashid ‘Baba Ubaya’, Cassian Ponera, Hassan Isihaka, Shaban Nditi, Ismail Aidan, Salehe Hamis/Ally Makalani dk 85, Kelvin Sabato, Awadh Juma/Juma Luizio dk63 na Salum Kihimbwa/Haroun Chanongo dk73.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NI SIMBA SC WASHINDI WA NGAO YA JAMII TENA, WAICHAPA MTIBWA SUGAR 2-1 KIRUMBA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top