• HABARI MPYA

    Friday, August 10, 2018

    ALLIANCE FC YAENDELEZA WIMBI LA USHINDI MECHI ZA KUJIANDAA NA MSIMU, YAICHAPA NA SINGIDA UNITED 2-1

    Na Mwandishi Wetu, MWANZA
    TIMU ya Alliance FC leo imeiadhibu Singida United baada ya kuichapa mabao 2-1 katika mchezo wa Kombe la Lake Zone PreSeason 2018 Uwanja wa Nyamagana mjini Mwanza.
    Mabaonya Alliance FC katika mchezo wa leo yamefungwa na Israel Patrick dakika ya tano na Maganda Mchembe dakika ya 39 wakati la Singida United limefungwa na John Tiber dakika ya 85.
    Huo unakuwa ushindi wa tatu mfululizo katika mechi zake za kujiandaa na msimu ujao wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, baada ya Alliance FC inayofundishwa na Kocha Mkuu, Mbwana Makatta kushinda 4-0 dhidi ya GIPCO ya Geita na 2-1 dhidi ya Kagera Sugar.

    Alliance FC ambayo kwa misimu miwili iliyopita imekuwa ikiikosakosa nafasi ya kupanda Ligi Kuu, hatimaye msimu huu imeitimiza ndoto zake na watakuwa miongoni mwa timu 20 zitakazocheza ligi hiyo.
    Ligi Kuu inatarajiwa kuanza Agosti 22 na Alliance watafungua dimba na mahasimu wao wa Jiji, Mbao FC Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza, huku Ruvu Shooting ikimenyana na Ndanda FC ya Mtwara Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani, na Coastal Union na Lipuli FC ya Iringa Uwanja wa Mkwakwani mjini Tanga. 
    Mechi nyingine ni kati ya Singida United na Biashara United Uwanja wa Namfua, Singida, Kagera Sugar na Mwadui FC Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba zote Saa 10:00 jioni na Simba SC na Tanzania Prisons Saa 1:00 usiku Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam. 
    Mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu utakamilishwa Agosti 23 kwa mechi kati ya JKT Ruvu na KMC Saa 8:00 mchana Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Stand United na African Lyon Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga, Mtibwa Sugar na Yanga SC Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro na Azam FC dhidi ya Mbeya City Saa 1:00 usiku.
    Ligi Kuu itafikia tamati Mei 19, mwakani (2019) ikiwa na jumla ya mechi 380 kutoka 240 msimu uliopita baada ya ongezeko la timu nne kutoka 16 za msimu uliopita.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ALLIANCE FC YAENDELEZA WIMBI LA USHINDI MECHI ZA KUJIANDAA NA MSIMU, YAICHAPA NA SINGIDA UNITED 2-1 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top