• HABARI MPYA

    Friday, February 02, 2018

    TEGETE: MECHI NA MBEYA CITY NI YA KUSHINDA KESHO MAJI MAJI

    Na Mwandishi Wetu, SONGEA
    MSHAMBULIAJI wa Maji Maji, Jerson John Tegete amesema kwamba mchezo wa nyumbani dhidi ya Mbeya City kesho Uwanja wa Maji Mji mjini Songea mkoani Ruvuma ni wa kushinda.
    Akizungumza na Bin Zubeiry Sports – Online mjini japa leo, Tegete amesema kwamba kuna mechi ngumu za kuzifikiria, lakini si dhidi ya Mbeya City.
    “Kuna mechi ngumu ukiwafikiria wapinzani tu kwa rekodi yao unaona kabisa unakenda kwenye mechi ngumu. Lakini si Mbeya City ya msimu huu. Hawana rekodi nzuri,”amesema Tegete.
    Jerry Tegete amesema mchezo dhidi ya Mbeya City kesho mjini Songea ni wa kushinda

    Amesema kwamba mchezo dhidi ya Mbeya City ni wa kushinda na ni mechi ambayo kama haushindi mwisho wa msimu unaweza kujuta.
    “Inatakiwa tujipange tushinde hii mechi lazima. Haiwezekani ufungwe na timu nzuri na hata timu kama Mbeya City pia ya msimu huu usiifunge,”amesema.
    Duru la pili la Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara linatarajiwa kuanza kesho kwa mechi tano kuchezwa kwenye viwanja tofauti nchini.   
    Uwanja wa Azam Complex, Chamazi mjini Dar es Salaam, wenyeji Azam FC wataikaribisha Ndanda FC ya Mtwara, Uwanja wa Samora mjini Iringa, mabingwa watetezi, Yanga SC watakuwa wageni wa Lipuli, Uwanja wa Namfua, Singida United wataikaribisha Mwadui FC ya Shinyanga, Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya, Tanzania Prisons watakuwa wenyeji wa Njombe Mji FC na Songea ni Maji Maji na Mbeya City.
    Ligi Kuu itaendelea Jumapili kwa mchezo mmoja tu kati ya Simba SC na Ruvu Shooting Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wakati Jumatatu kutakuwa na mechi mbili za kukamilisha mzunguko a 16; Stand United na Mtibwa Sugar Uwanja wa Kambarage na Mbao FC na Kagera Sugar ya Bukoba.
    Februari 8, Ruvu Shooting watakuwa wenyeji wa Kagera Sugar Uwanja wa Mabatini, Mlanduzi mkoni Pwani na Februari 12, Kagera Sugar watakuwa wenyeji wa Azam FC Uwanja wa Kaitaba, Bukoba.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TEGETE: MECHI NA MBEYA CITY NI YA KUSHINDA KESHO MAJI MAJI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top