• HABARI MPYA

    Monday, February 26, 2018

    SIMBA SC YAWATUMIA SALAMU WAARABU, YAWAPIGA MBAO FC 5-0 TAIFA

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    SIMBA SC imezidi kuukimbilia kwa kasi ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara baada ya ushindi wa mabao 5-0 dhidi ya Mbao FC ya Mwanza jioni ya leo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Mshambuliaji Mganda, Emmanuel Okwi alifunga mabao mawili moja kila kwa kipindi kabla ya kuumia na kutolewa wakati mabao mengine yalifungwa na Shiza Kichuya, Erasto Nyoni na Mghana, Nicholaus Gyan.
    Ushindi huo unaifanya Simba itimize pointi 45 baada ya kucheza mechi 19, ikiendelea kukaa kileleni mwa Ligi Kuu, ikifuatiwa na mabingwa watetezi, Yanga wenye pointi 37 za mechi 18, wakati Mbao FC inabaki nafasi ya 10 kwa pointi zake 19 za mechi 19.
    Emmanuel Okwi (kulia) akishangilia na Shiza Kichuya (katikati) na Muzamil Yassin baada ya kuifungia Simba bao la tatu
    Emmanuel Okwi akipasua msitu wa wachezaji wa Mbao FC 
    Shiza Kichuya (kushoto) akimtoka beki wa Mbao FC, Amos Charles 
    Beki Mghana wa Simba, Asante Kwasi akimtoka mchezaji wa timu yake ya zamani, Mbao FC
    Mshambuliaji wa Mbao FC, Habib Kiyombo akiwatoka wachezaji wa Simba

    Ili kuanza kupata mabao, benchi la Ufundi la Simba chini ya kocha Mfaransa, Pierre Lechantre anayesaidiwa na Mrundi, Masoud Juma lililazimika kufanya mabadiliko ya mapema kipindi cha kwanza katika safu ya kiungo kwa kumtoa Said Hamisi Ndemla na kumuingiza Muzamil Yassin baada ya nusu saa.
    Mabadiliko hayo yalibadilisha kabisa mwelekeo wa mechi, kutoka Mbao FC kutawala hadi Simba SC ambayo wiki ijayo itamenyana na El Masry ya Misri katika Raundi ya Kwanza ya kombe la Shirikisho Afrika kuuteka mchezo.    
    Shiza Ramadhani Kichuya akafungua sherehe za mabao za Simba kwa kufunga bao la kwanza dakika ya 38 akimalizia pasi ya mtokea benchi, Muzamil.
    Mganda Emmanuel Okwi akaifungia Simba SC bao la pili dakika ya 40 kwa penalti, baada ya yeye mwenyewe kuanguka kwenye boksi wakati anadhibitiwa na beki wa Mbao, David Mwasa.
    Refa Erick Onoka kutoka Arusha akawanyima Simba SC penalti sahihi zaidi ya aliyowapa mwanzo baada ya Okwi kuangushwa kwenye boksi na Nahodha wa Mbao FC, Mrundi, Yusuph Ndikumana ambaye leo alicheza chini ya kiwango.
    Kipindi cha pili, Mbao FC wanaofundishwa na kocha Mrundi, Etienne Ndayiragijje walikianza vizuri wakishambulia kujaribu kutafuta mabao ya kusawazisha, lakini safu ya ulinzi ya Simba chini ya kipa Aishi Salum Manula ilisimama imara.
    Kibao kikaigeukia Mbao FC na wakajikuta wanapachikwa mabao matatu ndani ya dakika 20, Okwi akianza kufunga dakika ya 69 kwa shuti la mguu wa kulia baada ya kupokea pasi ya Muzamil Yassin.
    Okwi anatolewa nje anachechemea baada ya kuumia kufuatia kugongana na beki wa Mbao FC, Amos Charles kwenye boksi na nafasi yake kuchukuliwa na Mrundi, Laudit Mavugo.   
    Beki mkongwe anayeweza kucheza kama kiungo pia, Erasto Edward Nyoni akaifungia Simba SC bao la nne dakika ya 82 kwa shuti la mpira wa adhabu kutoka umbali wa mita 19 kasoro kidogo, baada ya Muzamil kuangushwa.
    Refa Onoka akamtoa nje kwa nyekundu Nahodha wa Mbao FC, Ndikumana dakika ya 84 baada ya kumuonyesha kadi ya pili ya njano kufuatia kumchezea rafu Mavugo Mrundi mwenzake, Mavugo.
    Nicholaus Gyan akaifungia Simba SC bao la tano dakika ya 86 kufuatia krosi ya beki wa kulia, Shomary Kapombe kuzua kizaazaa langoni kwa Mbao FC. 
    Kikosi cha Simba SC; Aishi Manula, Shomari Kapombe, James Kotei, Yussuph Mlipili, Erasto Nyoni, Asante Kwasi, Jonas Mkude, Said Ndemla, Shiza Kichuya/Rashid Juma dk86, Nicholas Gyan na Emmanuel Okwi/Laudit Mavugo dk80.
    Mbao FC; Iyvan Rugumandiye, Boniphace Maganga, Amos Charles, David Mwasa, Yusuph Ndikumana, Ibrahim Njohole/ Said K. Said dk57, Herbet Lukindo, George Sangija, Habibu Hajji, James Msuva/Rajesh Kotecha dk51 na Emmanuel Mvuyekure/Ismail Ally dk70.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC YAWATUMIA SALAMU WAARABU, YAWAPIGA MBAO FC 5-0 TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top