• HABARI MPYA

    Wednesday, February 21, 2018

    NJOMBE MJI YAITOA MBAO FC KWA MATUTA AZAM SPORTS FEDERATION CUP

    MATOKEO/RATIBA AZAM SPORTS FEDERATION CUP
    Februari 21, 2018
    Njombe Mji 1-1 Mbao FC (Penalti 6-5)
    Februari 24, 2018
    Singida United v Polisi Tanzania Saa 10:00 jioni
    KMC v Azam FC Saa 1:00 usiku
    Februari 25, 2018
    Maji Maji  v Yanga SC Saa 10:00 jioni
    Buseresere v Mtibwa Sugar Saa 8:00 mchana
    Februari 26, 2018
    Kiluvya United v Tanzania Prisons         Saa 8:00 mchana 
    Stand United v Dodoma FC Saa 10:00 jioni
    Njombe Mji imekuwa timu ya kwanza kwenda Robo Fainali ya Azam Sports Federation Cup leo baada ya kuitoa Mbao FC

    Na Mwandishi Wetu, NJOMBE
    TIMU ya Mbao FC imetolewa kwenye michuano ya Azam Sports Federation Cup (ASFC) katika hatua ya 16 Bora tu baada ya kufungwa kwa penalti 6-5 kufuatia sare ya 1-1 na wenyeji, Njombe Mji FC ndani ya dakika 90 Uwanja wa Saba Saba mjini Njombe.
    Njombe walitangulia kwa bao la Ditram Nchimbi dakika ya 38, kabla ya Said Khamis kuisawazishia Mbao FC dakika ya 73.
    Na katika matuta, kinara wa mabao wa Mbao FC, Habib Kiyombo na Ibrahim Hashim walikosa penalti zao baada ya wenzao wote Herbet Lukindo, Emmanuel Mveyekule, Said Khamis, Amos Abel na Yusuph Ndikumana kufunga zilizotangulia.
    Waliofunga penalti za Njombe Mji FC ni Agathon Mapunda, David Kisu, Mustapha Bakari, Kennedy Masawe, Raphael Siame na Peter Mwangosi, wakati Ditram Nchimbi alikosa.
    Sasa timu zote zilizocheza fainali ya ASFC Mei 27, mwaka jana Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma zinaipa mgongo michuano hiyo hata kabla ya hatua ya Robo Fainali.
    Hiyo ni baada ya Simba, waliotwaa taji hilo kwa ushindi wa 2-1 kutolewa pia Desemba 22 kwa penalti 4-3, baada ya sare ya 1-1 ndani ya dakika 90 na timu ya Daraja la Pili, Green Warriors ya Mwenge, Dar es Salaam inayomilikiwa na Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) katika hatua ya 64 Bora.
    Hatua ya 16 Bora ya ASFC itaendelea zitaendelea Jumamosi Februari 24, wakati Singida United watakapowakaribisha Polisi Tanzania kwenye Uwanja wa Namfua saa 10 jioni na KMC watawaalika Azam FC saa 1 usiku Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.
    Jumapili Februari 25, 2018 Buseresere watakuwa uwanja wa Nyamagana Mwanza kucheza na Mtibwa Sugar ya Morogoro, Maji Maji FC ya Ruvuma watakuwa nyumbani kwenye uwanja wa Maji Maji mjini Songea kuwakaribisha Yanga SC ya Dar es Salaam wakati Ndanda FC watakuwa ugenini kucheza na JKT Tanzania Uwanja wa Azam Complex Chamazi.
    Jumatatu Februari 26, 2018 kutachezwa mechi mbili Kiluvya United dhidi ya Tanzania Prisons Uwanja wa Mabatini na Stand United watawaalika Dodoma FC  Uwanja wa Kambarage, Shinyanga.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NJOMBE MJI YAITOA MBAO FC KWA MATUTA AZAM SPORTS FEDERATION CUP Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top