• HABARI MPYA

    Friday, February 16, 2018

    LIPULI FC WANA SHUGHULI NZITO NA AZAM FC LEO SAMORA

    Na Mwandishi Wetu, IRINGA
    LIGI Kuu ya Vodacom Tanzania Bara inaendelea leo kwa mchezo mmoja, Azam FC wakiwa wageni wa Lipuli FC Uwanja wa Samora mjini Iringa.
    Azam FC leo watajaribu kusaka ushindi wa kwanza ndani ya mechi tatu, baada ya Jumatano ya Februari 7 kufungwa 1-0 na Simba SC Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kabla ya kutoa sare ya 1-1 na wenyeji, Kagera Sugar Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.
    Lakini upande wa Lipuli FC inayofundishwa na wachezaji wa zamani wa Simba SC, Amri Said na Suleiman Matola, wametoka kushinda mechi moja kati ya 10 zilizopita, wakifungwa tano na sare nne maana yake nao wana kiu ya ushindi.
    Lipuli FC wanaikaribisha Azam FC Uwanja wa Samora mjini Iringa leo katika mfululizo wa Ligi Kuu

    Kwa sababu hiyo unatarajiwa kuwa mchezo mzuri kwenye Uwanja mzuri na hali ya hali ya hewa nzuri mkoani Iringa. 
    Azam FC itaongezewa na wachezaji wake wawili iliyowakosa katika mechi mbili iliyopita, ambao ni Nahodha msaidizi Aggrey Moris, aliyekuwa akitumikiwa adhabu ya kadi tatu za njano na mshambuliaji Yahya Zayed, aliyeugua homa ghafla wakati timu hiyo ikielekea Bukoba kucheza na Kagera Sugar.
    Lakini Azam FC itaendelea kuwakosa nyota wake kadhaa akiwemo Nahodha, Himid Mao ‘Ninja’, aliyekwenda Afrika Kusini kwa matibabu ya goti lake la mguu wa kulia, beki Daniel Amaoh, ambaye ni majeruhi, mshambuliaji Waziri Junior, anayetarajiwa kufanyiwa upasuaji mdogo wa kifundo cha mguu na kiungo Salum Abubakar ‘Sure Boy’ aliyebaki Dar es Salaam kwa matatizo ya kifamilia.
    Pamoja na hayo, Kocha Mkuu wa Azam FC, Aristica Cioaba, amesema kikosi chake kipo kamili tayari kupambana na kuibuka na pointi zote tatu.
    Huo utakuwa ni mchezo wa tatu kwa timu hizo kukutana msimu huu, mechi moja ikiwa ni ya maandalizi ya msimu ambayo Azam FC ilishinda 4-0 mjini Iringa, mabao yaliyofungwa na beki Yakubu Mohammed, Zayed, Waziri Junior, Sure Boy huku ile ya pili ikiwa ni raundi ya kwanza ya ligi iliyopigwa Uwanja wa Azam Complex, na wenyeji hao kushinda 1-0 kwa bao lililofungwa na mshmbuliaji Mbaraka Yusuph aliyepokea pasi safi ya Himid.
    Hadi sasa ikiwa inaelekea raundi ya 19 ya mechi za ligi, Azam FC inashika nafasi ya tatu kwa pointi 34, ikizidiwa pointi tatu na Yanga (37) iliyo nafasi ya pili huku Simba ikiwa kileleni kwa pointi 42 baada ya sare ya mabao 2-2 waliyoipata leo dhidi ya Mwadui.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: LIPULI FC WANA SHUGHULI NZITO NA AZAM FC LEO SAMORA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top