• HABARI MPYA

    Saturday, February 25, 2012

    MAN CITY WAZIDI KUPAA ENGLAND

    MANCHESTER City imejitanua kileleni mwa Ligi Kuu ya England baada ya ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Blackburn Rovers kwenye Uwanja wa Etihad, mjini hapa leo.   Shukrani kwao Mario Balotelli aliyefunga dakika ya 30 kwa pasi ya Kolarov, Aguero aliyefunga dakika ya 52 kwa pasi ya David Silva na Dzeko aliyefunga dakika ya 81 kwa pasi ya Kolarov.
    Ushindi huo unaifanya City itemize pointi 63 baada ya kucheza mechi 26 na kujiachia kileleni kwa pointi tatu zaidi, dhidi ya mabingwa watetezi Man United wanaoshika nafasi ya pili. United wanacheza mechi yao ya 26 na Norwich City leo.
    Mapema leo, Chelsea iliibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Bolton na kufanikiwa kurejea ndani ya ‘top four’ kwenye Ligi Kuu ya England, sambamba na kumpunguzia jakamoyo kocha wake, Andre Villas-Boas.
    Shukrani kwao David Luiz, Didier Drogba na Frank Lampard kwa mabao yao ya kipindi cha pili, yaliyozima gundu la Chelsea kucheza mechi tano bila kushinda, hali ambayo ilikuwa inakiweka matatani kibarua cha kocha Villas-Boas.
    Ushindi huo unaifanya klabu hiyo ya London ipande nafasi ya nne, juu ya Arsenal.
    Bolton wanabaki kwenye ‘maeneo’ ya kushuka na wameshindwa kuvunja mwiko wa kutoifunga Chelsea tangu mwaka 2003.
    Katika mchezo mwingine, Wigan walilazimishwa sare ya bila kufungana na Aston Villa kwenye Uwanja wa DW Stadium.
    Aidha, bao pekee la Pavel Pogrebnyak lilitosha kuipa Fulham iliyocheza pungufu ya mchezaji mmoja ushindi wa 1-0 dhidi ya Queens Park Rangers kwenye Uwanja wa Loftus Road.
    Katika mchezo mwingine, West Bromwich Albion iliibuka na ushindi wa kwanza ndani ya miezi mitatu ilipoitandika mabao 4-0 nyumbani Sunderland 4-0.
    Wiki mbili tangu ipate ushindi mkubwa zaidi ugenini msimu huu wa mabao 5-1 dhidi ya Wolverhampton, West Brom ilipata mabao mawili kila kipindi dhidi ya Sunderland.
    Peter Odemwingie, aliyepiga mabao matatu peke yake dhidi ya Wolves, jana alifunga bao la mapema kabla ya James Morrison kufunga linguine kabla ya mapumziko na Keith Andrews, ambaye alicheza mechi ya kwanza dhidi ya timu yake ya zamani, Wolves alifunga dakika za lala salama.
    West Brom haikuruhusu nyavu zake kuguswa kwa mara ya kwanza ndani ya miezi miwili.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAN CITY WAZIDI KUPAA ENGLAND Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top