• HABARI MPYA

    Friday, August 03, 2018

    MVUA ZATIBUA MAANDALIZI YA SIMBA SC KAMBI YA UTURUKI…MECHI NA MABINGWA WA MOROCCO YAYEYUKA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MECHI ya kirafiki kati ya Simba na mabingwa wa Morocco, Ittihad Riadi de Tanger (IRT) uliokuwa ufanyike leo jioni mjini Istanbul, Uturuki umeahirishwa kwa sababu ya mvua na sasa utachezwa kesho asubuhi.
    Msemaji wa Simba SC, Hajji Sunday Manara amesema kwamba kutokana na mvua kubwa kunyesha leo mjini Istanbul, mchezo huo umeahirishwa na sasa utafanyika mapema kesho hali ikiruhusu.
    Mechi ya kwanza mabingwa hao wa Tanzania katika kambi yao ya Uturuki walitoka sare ya kufungana bao 1-1 na MC Oujder ya Morocco pia juzi jioni.

    Mechi kati ya Simba SC na Ittihad Tanger sasa itafanyika kesho asubuhi 

    Kikosi cha Simba SC kilichoweka kambi katika hoteli ya Reen Park & Resorts mjini Istanbul, kikifanya mazoezi yake katika moja ya viwanja saba vilivyoizunguka hoteli hiyo, kinatarajiwa kurejea nchini Agosti 5 tayari kwa tamasha la kila mwaka la klabu, Simba Day ambalo hufanyika Agosti 8 Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam.
    Na siku hiyo, Simba SC itamenyana na mabingwa mara mbili wa Afrika, Asante Kotoko ya Ghana  waliobeba taji hilo enzi za Klabu Bingwa Afrika katika miaka ya 1970 na 1983. 
    Wakati huo huo: Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye tamasha la Simba Day Agosti 8.
    Sambamba na hilo, Simba SC imetaja viingilio vya siku hiyo ambavyo ni Sh. 20, 000 kwa VIP A, Sh. 15, 000 kwa VIP B na Sh. 5,000 kwa majukwaa ya mzunguko.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MVUA ZATIBUA MAANDALIZI YA SIMBA SC KAMBI YA UTURUKI…MECHI NA MABINGWA WA MOROCCO YAYEYUKA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top