• HABARI MPYA

    Friday, February 03, 2017

    SERENGETI BOYS YAREJESHWA AFCON, KIJEBA AIPONZA KONGO

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    HATIMAYE timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 17 ya Tanzania, Serengeti Boys imerejeshwa kwenye michuano ya Mataifa ya Afrika kwa vijana wa umri huo.
    Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi akiwa mwenye furaha kubwa amesema jioni ya leo; "Timu ya Taifa ya vijana umri chini ya miaka 17 imefaulu kucheza fainali za Afrika. Hongera Serengeti Boys! Hongera Tanzania!,"amesema Malinzi na kufafanua.
    "Tumefaulu kucheza fainali za Afrika. Tulipeleka CAF malalamiko dhidi ya mchezaji wa Kongo Brazaville Langa Bercy kutilia mashaka umri wake. Aliitwa na CAF mara tatu arudie kipimo cha umri hakuja, hivyo Congo. imeondolewa kwenye mashindano," 
    Mwanzoni mwa mwezi uliopita, Shirikisho la Soka Afrika (CAF) liliwapa siku 10 Shirikisho la Soka Kongo (FECOFOOT) kumuwasilisha mchezaji Langa Lesse Bercy mjini Libreville, Gabon afanyiwe vipimo vya MRI ili kuthibitisha umri wake kama anaruhusiwa kucheza mashindano ya vijana chini ya umri wa miaka 17.
    Katika kikao cha Kamati ya Utendaji ya CAF jana mjini Libreville, FECOFOOT walitakiwa kumpeleka mjini humo Langa Lesse Bercy akafanyiwe vipimo kufuatia malalamiko yaliyowasilishwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), baada ya zoezi hilo kushindikana mara mbili.
    Na hatua hiyo ilifuatia Rufaa ya TFF dhidi ya mchezaji huyo baada ya Kongo kuitoa U-17 ya Tanzania katika hatua ya mwisho ya mchujo wa kuwania tiketi ya fainali za mwaka huu zilizopangwa kufanyika Madagascar.
    Awali, Kongo walitakiwa kumpeleka mchezaji huyo makao makuu ya CAF mjini Cairo, Misri kwa vipimo, lakini mara mbili wakashindwa kufanya hivyo.
    Fainali za U-17 Afrika ilikuwa zifanyike nchini Madagascar kuanzia Aprili mwaka huu, lakini mwezi uliopita CAF iliivua uenyeji na kutoa muda hadi Januari 30 mwaka huu nchi nyingine kujitokeza kuomba uenyeji.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SERENGETI BOYS YAREJESHWA AFCON, KIJEBA AIPONZA KONGO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top