• HABARI MPYA

    Friday, February 24, 2017

    HOMA YA PAMBANO LA WATANI, YANGA WAMGUNA REFA...SIMBA WAREJEA DAR

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    WAKATI Simba SC imerejea leo Dar es Salaam kutoka Zanzibar, wapinzani wao, Yanga wameonyesha kumtilia shaka refa Methew Akrama wa Mwanza.
    Simba wamewasili leo kwa ndege kutoka Zanzibar walipokuwa tangu Ijumaa iliyopita kwa maandalizi ya mchezo dhidi ya mahasimu wao, Yanga kesho Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Na baada ya Bin Zubeiry Sports – Online jana kufichua majina ya marefa watakaochezesha mechi hiyo ya mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, ambao ni Akrama katikati na Mohammed Mkono wa Tanga na Hassan Zani wa Arusha watakaopeperusha vibendera pembezoni mwa Uwanja, Yanga wameonyesha shaka.
    Katibu wa Yanga, Charles Boniface Mkwasa amewaambia Waandishi wa Habari leo kwamba wapinzani wao, Simba wanayo majina ya marefa hao muda mrefu.
    “Tunaheshimu maamuzi ya Kamati ya Waamuzi kwa kutaja majina ya marefa wa kusimamia mechi yetu ya kesho, lakini nasikitika kwamba haya majina yameanza kutajwa tangu jana na baadhi ya wapinzani wetu walikuwa nayo tangu jana na yamekuwa yakitajwa tajwa kwenye mitandao,”amesema Mkwasa.
    Pamoja na hayo, Nahodha na kocha huyo wa zamani wa Yanga, ameomba marefa hao wachezeshe kwa kufuata sheria 17, kwani vinginevyo watachafua amani Uwanja wa Taifa kesho.
    Mkwasa ameowamba pia mashabiki wa Yanga kesho wawe watulivu, kwa sababu Jeshi la Polisi limeahidi kuwa makini kuhakikisha hata marefa hawavurugi mchezo. “Polisi wamesema refa akijaribu kwenda kinyume kidogo, watamtoa,”amesema.  
    Yanga imeweka kambi eneo la Kimbiji, Kigamboni nje ya kidogo ya Jiji la Dar es Salaam tangu Jumatatu, wakati mahasimu wao, Simba walikuwa Zanzibar. 
    Katika mechi ya mzunguko wa kwanza, miamba hiyo ya soka ya nchini ilitoka sare ya 1-1 Oktoba 1, mwaka jana, Yanga wakitangulia kwa bao la Amissi Tambwe kipindi cha kwanza, kabla ya Simba kusawazisha kupitia kwa Shiza Kichuya kipindi cha pili.
    Hii ni mara ya pili kwa Akrama kuchezesha mechi ya watani, baada ya Oktoba 3, 2012 kuchezesha mechi ya Ligi Kuu pia timu hizo zikitoka sare ya 1-1 Uwanja wa Taifa. 
    Katika mchezo huo ulioanza Saa 1:02 usiku, Akrama alimtoa kwa kadi nyekundu winga Simon Msuva wa Yanga dakika ya 77 kwa kumrudishia rafu beki wa Simba, Juma Nyosso.
    Siku hiyo, Simba walitangulia kwa bao la kiungo Amri Kiemba dakika ya pili, kabla ya mshambuliaji Said Bahanuzi kuisawazishia Yanga dakika ya 63 baada ya beki Paul Ngalema kuunawa mpira kwenye boksi.
    Laini Akrama alilaumiwa kwa kumuonyesha kadi ya njano badala ya nyekundu kiungo wa Simba, Haruna Moshi ‘Boban’ alipomchezea rafu mbaya beki Kevin Yondan hadi akashindwa kuendelea na mchezo, na nafasi yake ikachukuliwa na Juma Abdul.
    Na pia alilaumiwa kuwa kutomchukulia hatua yoyote kipa Juma Kaseja aliyeonekana kupoteza muda tangu mwanzo, na alimpa onyo tu zaidi ya mara tatu.
    Haikuwa ajabu Oktoba 6 Akrama alipoondolewa kwenye orodha ya wamuzi wa kuchezeaha Ligi Kuu baada ya kuvurunda mechi hiyo namba 80, huku aliyekuwa mshika kibendera namba mbili, Ephrony Ndissa wa Dar es Salaam akipewa onyo. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HOMA YA PAMBANO LA WATANI, YANGA WAMGUNA REFA...SIMBA WAREJEA DAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top