• HABARI MPYA

    Wednesday, October 19, 2016

    TOTO NA YANGA; NGOMA YA BABA NA MWANA LEO KIRUMBA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MABINGWA watetezi, Yanga SC leo watakuwa wageni wa Toto Africans Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza katika mfululizo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Yanga SC inayoingia kwenye mchezo huo bila wachezaji wake watatu, kipa Ally Mustafa ‘Barthez’, beki Juma Abdul majeruhi na mshambuliaji Malimi Busungu mwenye matatizo ya kifamilia – inahitaji ushindi ili kupunguza wastani wa pointi inazozidiwa na vinara, Simba SC, nane.
    Kocha wa Yanga, Mholanzi Hans van der Pluijm amepania kushinda mchezo wa leo ili kutoongeza idadi ya pointi wanazozidiwa na Simba.  
    Yanga SC wanamenyana na Toto Africans Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza leo 

    Lakini Yanga itaingia kwenye mchezo huo ikitoka kulazimishwa sare na Azam FC Jumapili Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam.
    Kwa ujumla Ligi Kuu inatarajiwa kuendelea na mbali na Toto na Yanga - Azam FC watawakaribisha Mtibwa Sugar Uwanja wa Azam Complex, Ruvu Shooting watakuwa wenyeji wa Mwadui FC Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani, Ndanda FC wataikaribisha Mbeya City Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara na Prisons watakuwa wenyeji wa Stand United Uwanja wa Sokoine, Mbeya.
    Mechi nyingine za Jumatano, African Lyon wataikaribisha Maji Maji Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wakati Alhamisi Simba SC watakuwa wenyeji wa Mbao FC Uwanja wa Uhuru na JKT Ruvu wataikaribisha Kagera Sugar Uwanja wa Mabatini.
    Simba SC inagongoza Ligi Kuu sasa ikiwa imejikusanyia pointi 23 baada ya kucheza mechi tisa, ikifuatiwa na Stand United ya Shinyanga yenye pointi 20 za mechi 10, wakati mabingwa watetezi, Yanga wenye pointi 15 za mechi nane ni wa tatu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TOTO NA YANGA; NGOMA YA BABA NA MWANA LEO KIRUMBA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top