• HABARI MPYA

    Saturday, October 29, 2016

    SIMBA SC YAENDELEZA UBABE LIGI KUU, YAWAPIGA 3-0 MWADUI KAMBARAGE

    Na Mwandishi Wetu, SHINYANGA
    SIMBA SC imezidi kupiga kasi kuelekea kwenye taji la ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara baada ya jioni ya leo kuichapa Mwadui FC mabao 3-0 Uwanja wa Kambarage, Shinyanga.
    Ushindi huo unaifanya timu ya kocha Mcameroon, Joseph Marius Omog icheze mechi 12 za Ligi Kuu msimu huu bila kupoteza, ikishinda 10 na kutoa sare mbili.
    Aidha, matokeo hayo yanaifanya Simba SC ijinafasi kileleni mwa Ligi Kuu kwa kufikisha pointi 32, mbele ya mabingwa watetezi, Yanga SC wenye pointi 24 za mechi 11.  
    Shizza Kichuya amefunga bao lake la nane la msimu Ligi Kuu

    Katika mchezo wa leo, hadi mapumziko, Simba SC walikuwa wanaongoza kwa mabao 2-0, yote yakifungwa na viungo wapya waliosajiliwa kutoka Mtibwa Sugar.
    Mohammed ‘Mo’ Ibrahim alianza kufunga dakika ya 32 baada ya kumtoka beki wa Mwadui kufuatia pasi ya mshambuliaji Mrundi, Laudit Mavugo.
    Mo Ibrahim akamsetia Kichuya kuifungia Simba SC bao la pili dakika ya 45, hilo likiwa bao lake la nane msimu huu wa Ligi Kuu.
    Kipindi cha pili, Simba SC walirudi na moto ule ule na kufanikiwa kupata bao la tatu dakika ya 50, mfungaji Mo Ibrahim tena akimalizia pasi ya mshambuliaji wa zamani wa Mtibwa Sugar, Ame Ali.
    Kikosi cha Mwadui FC kilikuwa; Shabani Kado/Lucheke Mussa dk63, Iddy Mobby, David Luhende, Shaaban Aboma/Gerard Adam dk72, Joram Mgeveke, Abdallah Mfuko, Salim Khamis, Morris Kaniki, Paul Nonga, Rashid Ismail na Miraji Adam.
    Simba SC; Vincent Angban, Janvier Bokungu, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Method Mwanjali, Juuko Murshid, Jonas Mkude, Muzamil Yassin, Mwinyi Kazimoto/Ibrahim Hajib dk46, Laudit Mavugo/Ame Ali dk47, Shizza Kichuya/Said Ndemla dk66 na Mohamed ‘Mo’ Ibrahim.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC YAENDELEZA UBABE LIGI KUU, YAWAPIGA 3-0 MWADUI KAMBARAGE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top