• HABARI MPYA

    Sunday, October 30, 2016

    NI AGIZO LA KIGANJA ‘MBAYA WA MANJI’, AU AGIZO LA SERIKALI?

    WAKATI wa uchaguzi wa Yanga katikati ya mwaka huu kulitokea mvutano baina ya klabu hiyo, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na Baraza la Michezo la Taifa (BMT).
    Kwa pamoja TFF na BMT zilitaka kuusimamia na kuuongoza kikamilifu uchaguzi wa klabu hiyo, wakati Yanga ilitaka ifanye yenyewe mchakato huo.
    Katika mvutano huo, Mwenyekiti wa Yanga akaibuka na sauti zilizorekodiwa za watu aliodai ni viongozi wa TFF na BMT wakipanga njama za kumhujumu.
    Kwa tuhuma zile, ambazo baadaye ilidaiwa vielelezo vilipelekwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), BMT NA TFF wakakaa kando na Yanga ikafanya uchaguzi wake.
    Moja ya sauti zilizodaiwa kusikika katika mpango wa kutaka kumhujumu Manji kwenye uchaguzi ni ya Katibu wa BMT, Mohamed Kiganja.
    Na kwa bahati mbaya, hata siku moja Kiganja hajawahi kukana tuhuma hizo na kwa kitendo cha TFF na BMT na kujitoa na kuiacha Yanga ifanye uchaguzi wake yenyewe, iliwaaminisha wengi kweli kulikuwa kuna mpango wa kumhujumu Manji. 
    Wakati uchaguzi wa Yanga umepita na Manji ameshinda Uenyekiti wa klabu, BMT na klabu hiyo zinaingia katika mtafaruku mwingine.
    Yanga chini ya Manji wanadai BMT imekuwa ikikwamisha mambo mengi kuelekea kwenye mabadiliko ya uendeshwaji wa klabu.
    Na kutokana na BMT kugoma kuwapa ushirikiano viongozi wa Yanga, nao wameamua kujifanyia baadhi ya mambo bila kupitia Baraza hilo.
    Na mwisho wa siku, BMT hao hao wanadaiwa kuibuka kukwamisha mpango huo kwa kigezo cha taratibu kufuatwa – wakati wao wenyewe ndiyo wanatuhumiwa kukwamisha taratibu hizo.
    Wiki hii, Serikali iliwashauri wafanyabiashara wenye kutaka kujimilikisha klabu za Simba na Yanga kuanzisha timu zao kama mfanyabishara mwingine mkubwa nchini, Alhaj Sheikh Said Salim Awadh Bakhresa.
    Inafahamika, Mwenyekiti wa Yanga, Manji anataka kuikodisha klabu kwa miaka 10, wakati mfanyabiashara Mohamed ‘Mo’ Dewji anataka kununua asilimia 51 ya hisa za klabu ya Simba. 
    Na Katibu Mkuu wa BMT, Mohamed Kiganja alisema wiki hii mjini Dar es Salaam kwamba viongozi wa Simba na Yanga wanatakiwa kusitisha michakato yote inayoendelea ya kubadilisha umiliki wa timu kutoka kwa Wanachama kwenda katika umiliki wa hisa na ukodishwaji, hadi kutakapofanyika marekebisho ya Katiba zao.
    Kiganja alisema klabu hizo zinapaswa kurekebisha Katiba zao kwanza kabla ya kufanya mabadiliko hayo kwa mujibu wa Sheria ya Baraza hilo na Kanuni za Msajili namba 442 Kanuni 11 kifungu kidogo cha (1-9).
    Kiganja alisema kuwa mabadiliko hayo yanayoendelea kwenye Klabu hizo tayari yameingia dosari baada ya baadhi ya Wanachama kwenda Mahakamani kupinga michakato hiyo kitu ambacho sio kizuri na pia sio ishara nzuri endapo yataachwa yaendelee.
    Ni wanachama wa Yanga waliozuia mchakato wa mabadiliko ya klabu yao kwa kwenda Mahakamani kuzuia mkutano uliokuwa ufanyike mwishoni mwa wiki iliyopita Dar es Salaam. 
    Na Kiganja akasema mdau au mwanachama yeyote anayetaka kufanya uwekezaji kwenye Klabu hizo ni vema angeanzisha timu yake kama Bakhresa alivyoanzisha Azam FC ili kupunguza malalamiko kwa vile timu hizo zina Wanachama wengi.
    Kiganja alisema kuwa michakato hiyo ilitakiwa ianzie kwenye matawi nchi nzima ili maamuzi yawe ya wote, kwani mabadiliko yoyote ndani ya klabu hizo lazima yafuate Katiba zao.
    Kiganja anazungumzia mabadiliko ya Katiba yafanyike kwanza, wakati Yanga wamekuwa wakilalamika yeye amekuwa hataki kupitisha Katiba yao mpya.
    Yanga wanamlalamikia pia Kiganja kukwamisha mabadiliko ya Baraza la Wadhamini, ambao kimsingi ndiyo wanakuwa wamiliki wa klabu.
    Lakini wakati huo huo, kwa niaba ya Serikali Kiganja anapaza sauti kutaka taratibu zifuatwe ili kufikia mabadiliko – ni taratibu zipi zaidi ya zile anazodaiwa kuzikwamisha mfano upande wa Yanga?
    Pamoja na hayo, kuna rekodi ya tuhuma za Kiganja kuwa katika kambi ya kutaka kumhujumu Manji kwenye uchaguzi wa Yanga ambayo hajaifuta, kiasi kwamba wengi miongoni mwa wapenzi na wanachama wa klabu hiyo wameiamini.
    Rahisi tu kuona chochote atakachosema Kiganja dhidi ya Yanga itachukuliwa ni kwa saabu ya tofauti zake na Manji na hata kama maelezo yake yatakuwa yamebeba hoja za msingi zitapuuzwa.
    Hili nalo Serikali ilitazame.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NI AGIZO LA KIGANJA ‘MBAYA WA MANJI’, AU AGIZO LA SERIKALI? Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top