• HABARI MPYA

    Monday, October 24, 2016

    ULIMWENGU AACHANA NA TP MAZEMBE, AREJEA DAR KUJIPANGA KWENDA ULAYA

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Thomas Emmanuel Ulimwengu ‘Rambo’ amehitimisha miaka yake mitano ya kuitumikia klabu ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
    Ulimwengu amemaliza Mkataba wake wa miaka mitano wiki iliyopita na tayari yupo Dar es Salaam kwa mipango ya kuhamia klabu mpya, ambayo bila shaka itakuwa Ulaya.
    “Ninashukuru sana Mazembe, kwa miaka mitano imenikuza kisoka na kunifanya kwa ujumla nifurahie maisha ya soka na kuwa na ndoto na tamaa zaidi,”.
    Ulimwengu amehitimisha miaka yake mitano ya kuitumikia TP Mazembe ya DRC

    “Ningependa sana kubaki kwa sababu zote, lakini kwa kuwa inanibidi kujaribu kusaka changamoto mpya na mafanikio zaidi, nalazimika kufumba macho na kusonga mbele,”. 
    “Ila Mazembe daima itabaki kwenye mfuniko wa moyo wangu kama klabu ya kipekee katika historia ya maisha yangu ya soka,”amesema Ulimwengu akizungumza na BIN ZUBEIRY SPORTS – ONLINE leo.
    Kuhusu timu gani anakwenda baada ya kukataa kusaini Mkataba mpya Mazembe Ulimwengu amesema mambo yakatakapokuwa tayari atasema.
    Ulimwengu aliyezaliwa Juni 14, mwaka 1993 aliibukia katika taasisi ya soka Tanzania (TSA) mwaka 2008, kabla ya mwaka 2009 kwenda kuanza kukomazwa Ligi Kuu katika klabu ya Moro United alikokuwa akicheza kwa mkopo hadi mwaka 2010 alipokwenda akademi ya Athletic FC ya Sweden, alikocheza hadi 2011 TP Mazembe alipochukuliwa na timu ya vijana ya Mazembe.
    Alicheza U20 ya Mazembe kwa msimu moja kabla ya kupandishwa rasmi timu ya wakubwa mwaka 2012 na moja kwa moja kuwa mchezaji wa kikosi cha kwanza hadi anamaliza Mkataba.
    Ulimwengu anajivunia kushinda mataji makubwa akiwa na  Mazembe kama Ligi ya Mabingwa Afrika, Super Cup ya Afrika na pamoja na kucheza Klabu Bingwa ya Dunia.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ULIMWENGU AACHANA NA TP MAZEMBE, AREJEA DAR KUJIPANGA KWENDA ULAYA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top