• HABARI MPYA

    Sunday, October 02, 2016

    KUTOKA BAO LA MADARAKA 2002 HADI TAMBWE JANA, BADO TUNATAKA NINI?

    UWANJA wa Taifa, Dar es Salaam jana uligeuka kilinge cha mapambano baina ya Polisi na mashabiki wa Simba, wakati wa mchezo dhidi ya mahasimu wao, Yanga.
    Vurugu zilizuka dakika ya 26 jana katika mchezo huo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, baada ya mshambuliaji wa Yanga, Mrundi Amissi Joselyn Tambwe kuifungia bao la kuongoza timu yake katika sare ya 1-1.
    Tatizo halikuwa kufunga, bali lilikuwa bao la utata, kwani Tambwe alilalizimika kutumia mkono kuiweka sawa katika himaya yake pasi ya Mkongo, Mbuyu Twite kabla ya kumchambua kipa Muivory Coast, Vincent Angban.
    Wachezaji wa Simba walimfuata refa, Martin Saanya kulalamikia bao hilo na wakati huo huo mashabiki wao wakaanza kung’oa viti na kuvirusha uwanjani.
    Ikabidi Polisi waanze kupambana na mashabiki hao kwa kuwafyatulia moshi wa gesi za machozi ili kuwatuliza – jambo ambalo lilifanikiwa na mchezo ukaendelea hadi Shizza Ramadhani Kichuya alipoisawazisia Simba dakika ya 87.
    Lakini Saanya akajikuta katika wakati mgumu zaidi baada ya kumtoa kwa kadi nyekundu ya moja kwa moja, kiungo na Nahodha wa Simba, Jonas Gerald Mkude aliyekuwa mstari wa mbele katika kumghasi.
    Amani ilichafuka kwa muda fulani Uwanja wa Taifa, katika mchezo ambao ulihudhuriwa pia na Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Mchemba na Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe. 
    Kwa ujumla tukio la jana lilikumbushia tukio la Machi 31, mwaka 2002 katika fainali ya iliyokuwa michuano ya Kombe la Tusker baina ya watani hao wa jadi.
    Siku hiyo, Simba ilishinda 4-1 na refa Abdulkadir Omar ‘Msomali’ aliivuruga mechi na kuhatarisha amani uwanjani pia kwa madudu kama ya jana.
    Kwa nini? Katika mechi hiyo ya fainali iliyohudhuriwa na rais mstaafu wa awamu ya pili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Alhaj Ali Hassan Mwinyi, chupuchupu ivunjike dakika ya 32, baada ya Madaraka Suleiman kufunga bao ambalo kabla ya kufumua shuti lililomshinda kipa Manyika Peter, aliushika pia mpira kwa makusudi, ili kuuweka sawa. 
    Rais wa Yanga wakati huo, Tarimba Abbas aliinuka na kuwaonyesha ishara wachezaji wake watoke uwanjani na hapo ndipo meza kuu aliyokuwa ameketi mzee Mwinyi, ilipoanza kushambuliwa kwa chupa za maji na mashabiki wa Yanga. Abdulkadir Omar alisubiri hadi vurugu zilipotulizwa na FFU ndipo akaendeleza mchezo. Tarimba alitoka nje na hakutaka kuendelea kushuhudia mchezo huo. Baada ya hapo, alifungiwa na Chama cha Soka Tanzania, (FAT), sasa TFF kabla ya kujiuzulu uongozi wa klabu hiyo baadaye.
    Na hizi zinakuwa mechi mbili kati ya nyingi za watani wa jadi, ambazo zilivurugwa na marefa – hiki kikiwa kielelezo tosha waamuzi wa nyumbani si chaguo sahihi katika michezo ya aina hii.
    Nchi za wenzetu, mechi ya wapinzani wa jadi ni bidhaa kubwa na imepewa jina na kujengewa hadhi kubwa – mfano Hispania, wao wanaiita El Clasico.
    Najua Kenya, Uganda, Rwanda na nchi nyingine nyingi barani hata Sudan zingependa kuwa na mechi kama Simba na Yanga na bila shaka zingeijengea hadhi zaidi. 
    Wachambuzi mahiri wa soka Afrika, tayari wameiandika katika orodha ya mechi tano kali zaidi za wapinzani barani.
    Nyingine zikiwa ni kati ya Orlando Pirates na Kaizer Chiefs za Afrika Kusini na Al Ahly dhidi ya Zamalek za Misri.
    Hakuna ubishi kwamba upinzani wa Ahly na Zamalek huo ni dunia nzima - ni zaidi ya upinzani, lakini kwa Afrika fuatilia ligi nyingi, utagundua Simba na Yanga ni mechi yenye mvuto wa kipekee na ndiyo maana SuperSport walikuwa wanakuja kuionyesha ‘Live’ kabla ya Azam TV kununu haki za matangazo ya Ligi Kuu kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
    Pamoja na kubadilisha muundo wa soka yetu kutoka FAT hadi TFF na kutoka Ligi ya kuendeshwa na shirikisho lenyewe la soka nchini hadi Bodi maalum, lakini bado tumeshindwa kuifanya mechi ya watani iwe bidhaa yenye hadhi sawa na uzito wake.  
    Matokeo yake ni uharibifu unaotokea mara kwa mara na kuhatarisha usalama wa malefu wanaojitokeza viwanjani. 
    Tu, kwa sababu TFF inajua baada ya vurugu itazitaka fedha za kufidia uharibifu na faini klabu, imeshindwa kutafuta suluhisho la kudumu la matatizo ya kiuamuzi katika mechi za watani.
    Ukweli ni kwamba marefa wetu viwango vyao ni vidogo na wanahitaji changamoto zaidi ili kujiongeza – mojawapo ni kushuhudia waamuzi wa kigeni wakichezesha mechi ya watani wa jadi nchini.
    Marefa wa Tanzania hata wakipata nafasi ya kuchezesha mechi za CECAFA ni habari kubwa – kwenye mechi za CAF sana hupewa mechi za hatua za awali na tena kwa nadra na huwa mechi nyepesi.
    Na bado ukienda CAF utakuta skendo mbaya ya marefa fulani wa Tanzania (majina ninayahifadhi) kupokea rushwa ili kupanga matokeo na wamefutwa maisha kuchezesha mpira.  
    Rais wa TFF, Jamal Malinzi anajua kuhusu marefa wan chi hii tangu akiwa Katibu wa Yanga, lakini ajabu naye ameshindwa kuchukua hatua.
    Mechi ya jana imevurugwa na refa tu, hakuna kingine. Kutoka bao la Madaraka 2002 na uozo wa refa Abdulkadir hadi la Tambwe jana kichefuchefu cha refa Saanya – huu ni uthibitisho mwingine kwamba, marefa wazawa si chaguo sahihi kwa mechi za watani.        
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KUTOKA BAO LA MADARAKA 2002 HADI TAMBWE JANA, BADO TUNATAKA NINI? Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top