• HABARI MPYA

    Saturday, April 20, 2019

    SERENGETI BOYS YATUPWA NJE KINYONGE AFCON U17, YAPIGWA NA ANGOLA PIA 4-2 LEO

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    WENYEJI, Tanzania wametolewa kwenye Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika kwa vijana chini ya umri wa miaka 17 kwa kupoteza mechi zote tatu, kufuatia na leo jioni kufungwa mabao 4-2 na Angola katika mchezo wa mwisho wa Kundi A Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam.
    Bahati bahati mbaya zaidi hata jirani zao, Uganda nao wametupwa nje baada ya sare ya 1-1 na Nigeria katika mchezo mwingine wa mwisho wa Kundi A Uwanja wa Azam Complex, Chamazi mjini Dar es Salaam pia. 
    Maana yake, Nigeria iliyomaliza kileleni mwa kundi kwa pointi zake saba inaungana na Angola iliyomaliza na pointi sita kwenda Nusu Fainali na pia kujikatia tiketi ya fainali za Kombe la Dunia baadaye mwaka huu nchini Brazil.
    Katika mchezo wa leo, mabao ya Serengeti Boys yamefungwa na Omary Jumanne Omary dakika ya 12 na Agiri Aristides Ngoda dakika ya 44, wakati ya Angola yalifungwa na Telson Tome dakika ya 17, Osvaldo Capemba kwa penalti dakika ya 42, David Nzanza dakika ya 68 na Osvaldo Capemba dakika ya 72.
    Azam Complex kiungo John Kokas Alou alianza kuifungia Uganda dakika ya 69, kabla ya kiungo Ibraheem Olalekan Jabaar kuisawazishia Nigeria dakika ya 74.
    Mechi za mwisho za Kundi B zitachezwa kesho Guinea na Morocco Uwanja wa Taifa na Cameroon na  Senegal Azam Complex na zote zitaanza Saa 10:00 jioni.
    Cameroon inaongoza Kundi B kwa pointi zake sita ikifuatiwa na Guinea yenye pointi tatu, wakati Morocco na Senegal kila moja ina pointi moja.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SERENGETI BOYS YATUPWA NJE KINYONGE AFCON U17, YAPIGWA NA ANGOLA PIA 4-2 LEO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top