• HABARI MPYA

    Saturday, April 20, 2019

    SAMATTA AFUNGA KRC GENK YAENDELEZA ‘UMWAMBA’ UBELGIJI, YAICHAPA STANDARD LIEGE 3-1

    Na Mwandishi Wetu, LIEGE 
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Saamtta usiku wa jana amefunga bao moja, timu yake, KRC Genk ikiibuka na ushindi wa 3-1 dhidi ya Standard Liege katika mchezo wa hatua ya pili ya Ligi Daraja la Kwanza A Ubelgiji Uwanja wa Maurice Dufrasne mjini Liege.
    Samatta alifunga bao la pili dakika ya 53 akimalizia pasi ya kiungo wa kimataifa wa Ruslan Malinovskiy, kufuatia kiungo Bryan Heynen kufunga la kwanza dakika ya 42 akimalizia pasi ya mshambuliaji, Mbelgiji mwenzake, mshambuliaji Leandro Trossard.
    Bao la tatu la KRC Genk lilifungwa na Trossard dakika ya 80 safari hiyo naye akisetiwa na Heynen, wakati bao pekee la Standard Liege lilifungwa na kiungo Mromania, Razvan Gabriel Marin dakika ya  82 akimalizia pasi ya kiungo kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Merveille Bope Bokadi.
    Kipa Mmexico wa Standard Liege, Guillermo Ochoa akiwa amedaka mbele ya Mbwana Samatta wa KRC Genk jana

    Kwa ushindi huo wa nne katika mechi tano ikiwa imepoteza mchezo mmoja wa Championship Round baada ya kuongoza vizuri hatua ya kwanza ya ligi hiyo ijulikanayo kama Regular Season, Genk inajoongezea nafasi ya kutwaa ubingwa huku Samatta akizidi kukikaribia kiatu cha dhahabu baada ya kufunga bao la 22 la msimu.
    Kwa ujumla Samatta mwenye umri wa miaka 26, usiku huu ameifungia bao la 61 Genk akicheza mechi yake ya 151 kwenye mashindano tangu amejiunga nayo Januari mwaka 2016 akitokea TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
    Katika ligi ya Ubelgiji pekee amecheza mechi 118 sasa na kufunga mabao 46 na kwenye Kombe la Ubelgiji amecheza mechi tisa na kufunga mabao mawili na Europa League amecheza mechi 24 na kufunga mabao 14. 
    Kikosi cha Standard Liege kilikuwa; Ochoa, Vanheusden, Kosanovic, Cimirot, Carcela, Halilovic/Lestienne dk76, Marin, Djenepo, Fai, Laifis na Mpoku/Bokadi dk76.
    KRC Genk; Vukovic, Uronen, Lucumi, Dewaest, Maehle, Heynen, Berge, Malinovskyi/Wouters dk86, Ito, Trossard/Ndongala dk87 na Samatta.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA AFUNGA KRC GENK YAENDELEZA ‘UMWAMBA’ UBELGIJI, YAICHAPA STANDARD LIEGE 3-1 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top