• HABARI MPYA

    Thursday, March 01, 2018

    GWIJI WA SIMBA ARTHUR MAMBETA AFARIKI DUNIA DAR

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    GWIJI wa klabu ya Simba, Arthur Mambeta amefariki dunia Jumatano baada ya kusumbuliwa na maradhi ya saratani kwa muda mrefu.
    Mambeta alianza kuchezea Simba SC miaka ya 1960 enzi za Sunderland na wakati wake alikuwa kiungo mshambuliaji hodari kuanzia klabu yake hadi timu ya taifa. 
    Kocha wa Tanzania miaka hiyo, Milan Celebic raia wa Yugoslavia aliwahi kusema kwamna kuunda timu ya taifa bila ya Arthur Mambeta ni sawa na kula chakula bila ya chumvi au chai iliyokisa sukari
    Arthur Mambeta (juu kulia) akiwa na magwiji wengine wa Simba wa miaka tofauti. Kushoto kwake ni Abdallah Msamba (marehemu pia) na chini, kulia ni Zamoyoni Mogella na kushoto Abdallah Kibadeni
    Na Arthur Mambeta ndiye mchezaji pekee wa Tanzania aliyekuwemo kwenye kikosi cha kwanza cha kombaini ya Afrika Mashariki iliyocheza na West Bromwich Albion ya England mwaka 1974 Uwanja wa Nakivubo mjini Kampala, Uganda.
    Katika mechi hiyo mchezaji mwingine wa Tanzania aliyeteuliwa, Kitwana Manara alikuwa bechi kama kipa wa akiba kabla ya kuhamia kwenye ushambuliaji ambako pia alikuwa tishio hadi anastaafu soka.
    Baada ya kustaafu soka, Mambeta alindelea kujihusisha na mchezo katika utawala na amewahi kuteuliwa katika nafasi mbalimbali za uongozi Simba SC.
    Hata hivyo, Mambeta alianza kujitoa taratibu kwenye soka baada ya kuanza kusumbuliwa na maradhi ya saratani yaliyosababisha akatwe miguu yake yote miwili. 
    Taarifa zaidi kuhusu msiba huo na taratibu zake zinataolewa kutolewa na familia ya marehemu Alhamisi. Mungu ampumzishe kwa amani marehemu Arthur Mambeta. Amin.

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: GWIJI WA SIMBA ARTHUR MAMBETA AFARIKI DUNIA DAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top