• HABARI MPYA

    Monday, October 03, 2016

    SERENGETI BOYS KUREJEA KESHO BAADA YA KUTOLEWA NA KONGO BRAZZAVILLE

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 20, Serengeti Boys inatarajiwa kurejea nchini kesho Saa 3:00 usiku kutoka Brazzaville, Kongo.
    Serengeti Boys ilikosa nafasi ya kwenda fainali za U-17 Afrika mwakani Madagascar, baada ya kutolewa na wenyeji, Kongo-Brazzaville kwa bao la ugenini.
    Jana Serengeti Boys ilifungwa 1-0 Uwanja wa Kumbukumbu ya Alphonse Massamba-Debat mjini Brazaville na kuwa sare ya jumla ya 3-3, hivyo Kongo kunufaika na mabao waliyofunga Dar es Salaam Tanzania ikishinda 3-2.
    Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Emil Malinzi amesema leo kwamba baada ya mechi vijana walilia sana jana.
    “Imeumiza, lakini ndio mpira. Timu itatua kesho na Jumatano tutakula nao chakula cha mchana na kuwaeleza nini matarajio yetu kwao,”amesema Malinzi.
    Rais huyo wa TFF, amesema kwamba Serengeti Boys ndiyo itakuwa timu ya vijana chini ya umri wa miaka 20, Ngorongoro Heroes mwaka 2019.
    “Taratibu tutajenga Taifa Stars ya 2021 kwa kuwashirikisha kwa karibu vijana hawa. Kikubwa ni sisi viongozi kutokaa nao mbali na kuzidi kuwapatia mechi hasa za kimataifa, ni muhimu wakue pamoja.” amesema.
    Malinzi pia amesema maandalizi ya kikosi cha U-17 kitakachoiwakilisha Tanzania kwenye fainali za Afrika mwaka 2019 ambazo tutakuwa wenyeji yanaendelea.
    “Mwezi Desemba watacheza mechi yao ya kwanza ya kimataifa. Ni vyema wajitambue mapema kuwa wao ni wawakilishi wa nchi,”amesema Malinzi kuhusu timu hiyo ambayo ipo kambini Mwanza.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SERENGETI BOYS KUREJEA KESHO BAADA YA KUTOLEWA NA KONGO BRAZZAVILLE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top