• HABARI MPYA

    Wednesday, November 08, 2017

    SIMBA KUCHEZA MECHI NYINGINE SUMBAWANGA KESHO

    Na Rehema Lucas, DAR ES SALAAM
    BAADA ya sare ya 0-0 na Nyundo FC jana Uwanja wa Azimio, Mpanda mkoani Katavi, Simba SC imeondoka leo asubuhi kwenda Sumbawanga, ambako kesho watakuwa na mchezo mwingine wa kirafiki.  
    Nyundo FC inayoshiriki Ligi Daraja la Pili Tanzania Bara, jana iliwafurahisha mashabiki wa nyumbani kwenye Uwanja wa Azimio kwa soka safi na kuwabana vinara wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kwa sare ya 0-0.
    Kocha Mcameroon Joseph Omog ameridhishwa na viwango vya wachezaji ambao wamekuwa hawapati nafasi mara kwa mara kikosini, baada ya wachezaji wengi wa kikosi cha kwanza kwenda kwenye timu zao za taifa.  
    Lakini kilikuwa kikosi imara kikiundwa na viungo mahiri, Mwinyi Kazimoto, Muzamil Yassin, Mohammed Ibrahim na washambuliaji, Mrundi Laudit Mavugo na Mghana, Nicholas Gyan ambacho kilishindwa kuonyesha cheche kwenye Uwanja wa uzio wa fito.   
    Na sasa kikosi kinaelekea Sumbawanga ambako kesho kitakuwa na mechi nyingine ya kirafiki, kabla ya Ijumaa kurejea Mbeya kuendelea na maandalizi ya mchezo wake ujao wa Ligi Kuu dhidi ya Tanzania Prisons Novemba 18 Uwanja wa Sokoine.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA KUCHEZA MECHI NYINGINE SUMBAWANGA KESHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top