• HABARI MPYA

    Thursday, November 23, 2017

    MECHI YA SIMBA NA LIPULI YARUDISHWA UWANJA WA UHURU

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MCHEZO wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kati ya Simba SC na Lipuli ya Iringa uliokuwa uchezwe Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam umerudishwa Uwanja wa Uhuru.
    Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniphace Wambura amesema hayo katika mkutano na Waandishi wa Habari ofisi za shirikisho hilo zilizopo Uwanja wa Karume, Dar es Salaam.
    Wambura alisema awali wamiliki wa Uwanja wa Uhuru walisema Jumamosi na Jumapili Uwanja huo utakuwa na shughuli nyingine, lakini jana wakawaambia Jumapili Uwanja utakuwa wazi hivyo wakaamua kuurudisha mchezo wa Simba kwenye Uwanja huo.
    Mchezo kayi ya Yanga SC na Tanzania Prisons ya Mbeya wenyewe utachezwa Chamazi kama ilivyoelezwa awali.
    Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara itaendelea kesho, wenyeji Ndanda FC wakiwakaribisha Njombe Mji FC Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara na Jumamosi mbali ya Yanga kuikaribisha Tanzania Prisons Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam na  Singida United watakuwa wenyeji wa Mbeya City Uwanja wa Namfua, Singida.
    Mechi nyingine za jumamosi, Mbao FC wataikaribisha Mwadui FC Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza, Kagera Sugar wataikaribisha Stand United Uwanja wa kambarage Shinyanga na Ruvu Shooting watakuwa wenyeji wa Maji Maji Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani. 
    Mzunguko wa 11 wa Ligi Kuu inayoonyeshwa moja kwa moja na Televisheni ya Azam TV utakamilishwa Jumatatu ijayo kwa mchezo mmoja kati ya wenyeji, Azam FC na Mtibwa Sugar Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MECHI YA SIMBA NA LIPULI YARUDISHWA UWANJA WA UHURU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top