• HABARI MPYA

    Sunday, June 12, 2016

    TELELA ATEMWA RASMI YANGA, TINOCCO ATOLEWA KWA MKOPO

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
    KIPA Benedictor Tinocco atatolewa kwa mkopo, wakati kiungo Salum Abdul Telela hataongezewa Mkataba Yanga.
    Habari za ndani ambazo BIN ZUBEIRY SPORTS – ONLINE imezipata kutoka Yanga zimesema kwamba maamuzi hayo yamepitishwa na kocha Mholanzi, Hans van der Pluijm.
    “Tinocco atatolewa kwa mkopo sehemu ambayo anaweza kupata nafasi ya kucheza, ili kama atapandisha uwezo wake, anaweza kurudishwa, lakini Telela kocha (Pluijm)” kimesema chanzo kutoka Yanga.
    Bado haijafahamika haswa sababu za Telela kutoongezewa Mkataba, licha ya umuhimu wake wa wazi unaoonekana katika timu kwa sababu ni kiraka anayeweza kucheza kama beki wa kulia, kati na nafasi zote za kiungo.
    Fundi Salum Telela ameachwa Yanga SC licha ya kwamba bado ni mchezaji muhimu katika timu

    Na kuhusu suala la nidhamu, Telela anaonekana ni mchezaji mwenye nidhamu, bidii ya mazoezi na kujituma, ambaye wakati wote anapoingizwa uwanjani licha ya muda mwingi kuwa mchezaji wa akiba hucheza vizuri. 
    Wakati huo huo, Yanga inaendelea kusubiri ofa ya kumuuza mshambuliaji Paul Nonga ambaye ameombwa mwenyewe kuuzwa, ili kwenda timu ambayo atakuwa anacheza.
    Nonga aliyesajiliwa Desemba kwa dau la Sh. Milioni 20 kutoka Mwadui FC ya Shinyanga ameamua kuondoka baada ya kushindwa ushindani wa namba.
    Washambuliaji chaguo la kwanza wa Yanga ni Mzimbabwe Donald Ngoma na Mrundi, Amissi Tambwe wakati Nonga alikuwa wa akiba pamoja na Malimi Busungu na Matheo Anthony.  
    Tayari Yanga SC imekwishamuacha kiungo kutoka Niger, Issoufou Boubacar ambaye pia alisajiliwa dirisha dogo Desemba.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TELELA ATEMWA RASMI YANGA, TINOCCO ATOLEWA KWA MKOPO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top