• HABARI MPYA

    Wednesday, March 26, 2014

    YANGA SC YAIKANDAMIZA PRISONS 5-0 TAIFA, UBINGWA BARA BADO HAUNA MWENYEWE

    Na Zaituni Kibwana, Dar es Salaam
    YANGA SC imeiadhibu vikali Prisons ya Mbeya kwa kuichapa mabao 5-0 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam jioni hii.
    Ushindi huo unaifanya Yanga SC iendelee kuwa na matumaini ya kutetea taji lake, kwani sasa inatimiza pointi 46 baada ya mechi 21, ikizidiwa pointi nne na Azam FC walio kileleni. 
    Katika mchezo huo, uliochezeshwa na refa Andrew Shamba wa Pwani, aliyesaidiwa na Charles Mbilinyi wa Mwanza na Said Mnonga wa Mtwara, hadi mapumziko, tayari Yanga SC walikuwa mbele kwa mabao 2-0.
    Wachezaji wa Yanga SC wakimpongeza Hamisi Kiiza wa pili kushoto aliyefunga mabao mawili leo

    Mshambuliaji Mganda, Emmanuel Arnold Okwi aliifungia Yanga SC bao la kwanza dakika ya 20 kwa shuti la chini la mpira wa adhabu, baada ya yeye mwenyewe kuangushwa nje kidogo ya boksi.
    Prisons ilipata nafasi ya kusawazisha bao hilo dakika ya 38, baada beki wa kushoto wa Yanga SC, Oscar Joshua kumsukuma kwenye eneo la hatari Frank Hau, lakini Lugano Mwangama akakosa penalti kwa kupiga juu ya lango la Juma Kaseja.
    Mrisho Khalfan Ngassa aliiunganisha nyavuni moja kwa moja vizuri krosi ya Hussein Javu dakika ya 37 kuipatia Yanga SC bao la pili. Kocha Mholanzi wa Yanga SC, Hans van der Pluijm alifanya mabadiliko dakika ya 33 kwa kumtoa Jerry Tegete na kumuingiza Hussein Javu. 
    Mrisho Ngassa wa Yanga SC kushoto akitafuta mbinu za kumtoka beki wa Prisons, Laurian Mpalile kulia
    Naipenda Yanga SC; Mrisho Ngassa kushoto akishangilia baada ya kufunga

    Kipindi cha pili, Yanga SC walirudi na moto na wao na kufanikiwa kupata mabao matatu zaidi.
    Hamisi Kiiza aliyeingia kuchukua nafasi ya Okwi, aliifungia Yanga SC bao la tatu dakika ya 67 akiunganisha krosi ya Simon Msuva.
    Nahodha Nadir Haroub ‘Cannavaro’ aliifungia Yanga SC bao la nne dakika ya 76 kwa penalti, kufuatia Hussein Javu kuangushwa na Nurdin Chona kwenye eneo la hatari. 
    Diego wa Uganda, Hamisi Kiiza aliifungia Yanga SC bao la tano akimalizia krosi ya Msuva dakika ya 88. Kipindi cha kwanza, Prisons kidogo ilionyesha uhai, lakini kipindi cha pili ilijifia kabisa na Yanga ‘wakamsukuma mlevi’.  
    Kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Juma Kaseja, Juma Abdul, Oscar Joshua, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan, Frank Domayo, Simon Msuva, Hassan Dilunga, Jerry Tegete/Hussein Javu dk33, Mrisho Ngassa/Haruna Niyonzima dk76 na Emmanuel Okwi/Hamisi Kiiza dk59.
    Prisons; Beno Kakolanya, Salum Kimenya, Laurian Mpalile, Lugano Mwangama, Nurdin Chona, Jumanne Elfadhil, Godfrey Mageta/Jimmy Shoji dk68, Freddy Chudu, Peter Michael, Frank Hau na Ibrahim Mamba/Six Mwakasega dk48. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC YAIKANDAMIZA PRISONS 5-0 TAIFA, UBINGWA BARA BADO HAUNA MWENYEWE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top