• HABARI MPYA

    Friday, March 28, 2014

    MECHI NA SIMBA SC ITAKUWA NGUMU- AZAM FC

    Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
    AZAM FC imesema kwamba, mechi na Simba SC Jumapili itakuwa ngumu kwa sababu wapinzani wao bado ni timu bora na watataka kurejesha heshima baada ya kucheza mechi tano bila kushinda.
    Katibu wa Azam FC, Nassor Idrisa ‘Father’ amesema katika mahojiano na tovuti ya klabu kwamba, wanaiheshimu Simba SC kama moja ya timu za kihistoria nchini na pia ni timu bora, hivyo wanaamini wanaingia kwenye mchezo mwingine mgumu.

    “Simba SC ni moja ya timu bora msimu huu, haipo kwenye mbio za ubingwa kwa sababu ya bahati tu, lakini si kama  ni timu mbaya. Kumbuka tulikuwa na Simba SC katika Kombe la Mapinduzi mapema mwaka huu, sisi tukatolewa Nusu Fainali, wao wakaingia Fainali,”alisema Father.
    Ameongeza kwamba, kuelekea mchezo huo, maandalizi yanaendelea vizuri na timu ipo kambini katika hosteli za Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.
    Baada ya ushindi wa 2-0 juzi ugenini dhidi ya timu isiyofungika Uwanja wa Mkwakwani, Tanga, kikosi cha Joseph Marius Omog kilirejea Dar es Salaam jana na leo kitaendelea na mazoezi kujiandaa na mchezo wa Jumapili.
    Azam FC ipo kileleni mwa Ligi Kuu kwa pointi zake 50 ilizovuna katika mechi 22, ikifuatiwa na mabingwa watetezi, Yanga SC wenye pointi 46, lakini wana mchezo mmoja mkononi. Wakati Yanga SC imebakiza mechi tano na Azam FC nne, mchuano wa kuwania ubingwa unaonekana kuwa mkali baina ya timu hizo mbili na mechi za Jumapili zinatarajiwa kutoa picha zaidi ya mbio zao.
    Azam FC ikiwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kumenyana na Simba SC, wapinzani wao katika mbio za ubingwa, Yanga SC watahamia Mkwakwani, Tanga kuwakabili Mgambo JKT.  
    CHANZO;www.azamfc.co.tz
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MECHI NA SIMBA SC ITAKUWA NGUMU- AZAM FC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top