• HABARI MPYA

    Saturday, March 29, 2014

    TOFAUTI YA MRISHO NGASSA WA YANGA SC NA YULE WA SIMBA SC MSIMU ULIOPITA...

    Na Mahmoud Zubeiry, Dar es Salaam
    MRISHO Khalfan Ngassa kesho atatimiza idadi ya mechi ambazo alicheza Simba SC, (27) msimu uliopita, wakati Yanga SC itakapomenyana na Mgambo JKT Uwanja wa Mkwakwani, Tanga lakini Jangwani amefanya mambo makubwa zaidi.
    Kwa msimu mzima uliopita Mrisho Ngassa akiwa Simba SC alifunga mabao saba tu katika mechi 27, wakati sasa Ligi Kuu ikiwa inaelekea ukingoni, mchezaji huyo amekwishafunga mabao 17 katika mechi 26.
    Hapa ndiyo kwangu; Mrisho Ngassa akiwapa ishara mashabiki wa Yanga SC baada ya kufunga bao lake la 17 tangu arejee timu hiyo msimu huu dhidi ya Prisons Jumatano Uwanja wa Taifa.

    Mabao tisa amefunga katika Ligi Kuu, wakati mengine amefunga katika Ligi ya Mabingwa Afrika na mechi za kirafiki.
    Ikumbukwe Ngassa aliuanzia nje msimu huu, akikosa mechi sita baada ya kufungiwa na Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa kubaini alisaini Yanga SC akiwa ana mkataba na Simba SC pia.
    Ngassa alitua Simba SC msimu uliopita akitokea Azam FC ambao walimtoa kwa mkopo baada ya kukerwa na tabia zake na Kamati pia ilimuauru kurudisha Sh. Milioni 30 alizochukua kusaini Mkataba na Wekundu wa Msimbazi pamoja na fidia ya asilimia 50 (sh. milioni 15).
    Ngassa aliichezea Simba SC mechi 27 msimu uliopita na kuifungia mabao saba tu
    Ngassa hakucheza mechi ya Ngao ya Jamii dhidi ya Azam na akakosa mechi tano za mwanzo za Ligi Kuu, lakini pamoja na hayo ana mabao tisa kwenye ligi hiyo pekee, nyuma ya Hamisi Kiiza aliyefunga mabao 11, akiwa mchezaji wa Yanga SC mwenye mabao mengi zaidi katika Ligi, anazidiwa na kinara Amisi Tambwe wa Simba SC mabao sita.
    Mchezaji mwenzake wa zamani; Ngassa alicheza pamoja na Ramadhani Singano 'Messi' katika kikosi cha Simba SC msimu uliopita.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TOFAUTI YA MRISHO NGASSA WA YANGA SC NA YULE WA SIMBA SC MSIMU ULIOPITA... Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top