• HABARI MPYA

    Sunday, March 23, 2014

    COASTAL UNION YAIADHIRI SIMBA SC DAR, YAICHAPA 1-0 TAIFA

    Na Baby Akwitende, Dar es Salaam
    SIMBA SC imelala bao 1-0 nyumbani mbele ya Coastal Union ya Tanga katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Hadi mapumziko, tayari Coastal walikuwa mbele kwa bao hilo 1-0 lililofungwa na beki wa kulia Hamad Juma dakika ya 44 aliyefumua shuti akiwa ndani ya boksi baada ya kupokea pasi ya kiungo Razak Khalfan.
    Kiungo Henry Joseph alionyeshwa kadi ya njano dakika ya 19 na refa Simon Mbelwa kwa kucheza rafu na dakika tatu baadaye kocha Mcroatia Zdravko Logarusic akamtoa mchezaji huyo na kumuingiza kinda Said Ndemla.
    Beki wa Coastal, Hamad Juma kushoto akimfukuza Haroun Chanongo wa Simba SC leo
    Hamad Juma kushoto akimdhibiti Ramadhani Singano 'Messi'
    Simba na Coastal wakionyeshana kazi leo Taifa

    Simba SC ilicharuka tangu baada ya kufungwa na kutengeneza nafasi nyingi za kufunga, lakini wakashindwa kuzitumia, wakati Coastal ilicheza kwa kujihami zaidi baada ya bao lao.
    Kwa matokeo hayo, Coastal inafikisha pointi 29 baada ya kucheza mechi 21 na kupanda hadi nafasi ya tano, wakati Simba SC inabaki nafasi ya nne kwa pointi zake 36 za mechi 22.
    Kikosi cha Simba SC leo kilikuwa; Ivo Mapunda, Haruna Shamte/Edward Christopher dk62, Issa Rashid ‘Baba Ubaya’, Joseph Owino, Donald Mosoti, Henry Joseph/Said Ndemla dk22, Omar Salum/William Lucian ‘Gallas’ dk46, Jonas Mkude, Haroun Chanongo, Amisi Tambwe na Ramadhani Singano ‘Messi’.
    Coastal Union; Fikirini Suleiman, Hamad Juma/Ayoub Masoud dk60, Abdi Banda, Yussuf Chuma, Mbwana Hamisi, Razak Khalfan, Ally Nassor/Mohamed Mtindi dk35, Behewa Sembwana, Suleiman Kassim ‘Selembe’, Daniel Lyanga na Keneth Masumbuko. 
    Katika mechi nyingine, Azam FC imeifunga JKT Oljoro 1-0 Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam bao pekee la John Bocco ‘Adebayor’ dakika ya 71, Ruvu Shooting imeifunga 2-0 Ashanti United Uwanja wa Mabatini, Mlandizi, Pwani mabao ya Elias Maguri dakika za sita na 63 wakati Mgambo JKT imetoka sare ya 1-1 na Mtibwa Sugar ya Morogoro Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: COASTAL UNION YAIADHIRI SIMBA SC DAR, YAICHAPA 1-0 TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top