• HABARI MPYA

    Tuesday, August 20, 2019

    KMC YAOMBA MASHABIKI WAJITOKEZE KWA WINGI IJUMAA KUWASAPOTI WAIPIGE AS KIGALI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    WACHEZAJI wa timu ya Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni (KMC) wamewaomba wapenzi wa soka kujitokeza kwa wingi Ijumaa Uwanja wa Taifa mjini Dar ers Salaam kuwasapoti katika mchezo wa marudiano Raundi ya Kwanza Kombe la Shirikisho dhidi ya AS Kigali ya Rwanda.
    KMC watakuwa wenyeji wa AS Kigali, timu mpya ya kiungo wa zamani wa Yanga na Simba, Haruna Niyonzima keshokutwa katika mchezo wa marudiano Raundi ya Kwanza Kombe la Shirikisho, wakihitaji ushindi wowote kusonga mbele baada ya sare ya 0-0 kwenye mchezo wa kwanza Rwanda. 
    Wakizungumza kwa niaba ya wenzako, nyota wa KMC, kiungo Hassan Kabunda na mshambuliaji James Msuva wamewaomba wapenzi kujitokeza kwa wingi Ijumaa Uwanja wa kuwasapoti.
    “Kwa maandalizi yetu, timu kama KMC tumekwishamaliza kazi, kilichobaki ni kuwaua AS Kigali, tunawauaje, tunahitaji sapoti yenu mashabiki, bila sapoti yenu sisi hamna kitu, KMC pamoja na mashabiki kinakuwa kitu kimoja, ndiyo mwisho wa siku tunasema Pamoja tunaweza,”amesema Msuva, mdogo wa kiungo mshambuliaji wa Difaa Hassan El Jadidi ya Morocco, Simon Msuva.
    Kwa upande wake Kabunda, mtoto wa beki wa zamani wa kimataifa wa Tanzania, Salum Kabunda ‘Ninja’ amesema; “Tuna imani kabisa tutawafunga AS Kigali, tunachoomba mashabiki tu waje kwa wingi Ijumaa watupe sapoti,”.
    KMC iliyopanda Ligi Kuu ya Tanzania Bara msimu uliopita, moja kwa moja imetokea kuwa moja ya timu tishio nchini na msimu imepata tiketi ya kucheza Kombe la Shirikisho baada ya kumaliza nafasi ya nne kwenye msimamo, nyuma ya Azam FC.
    Bingwa na mshindi wa pili wanacheza Ligi ya Mabingwa Afrika, wakati mshindi wa tatu anaungana na mshindi wa Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kucheza Kombe la Shirikisho. 
    Na kwa kuwa Azam FC ndiye mshindi wa Kombe la TFF, maarufu kama Azam Sports Federation Cup (ASFC), KMC imepata nafasi ya kushiriki Kombe la Shirikisho Afrika pamoja na kumaliza nafasi ya nne. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KMC YAOMBA MASHABIKI WAJITOKEZE KWA WINGI IJUMAA KUWASAPOTI WAIPIGE AS KIGALI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top