• HABARI MPYA

    Monday, August 26, 2019

    HONGERA YANGA SC KWA KUITOA ROLLERS, LAKINI ILI KUITOA ZESCO...

    Na Dominick Salamba, DAR ES SALAAM
    KUNA msanii mmoja wa Bongo Fleva ile ya zamani kidogo wakati nipo kwenye ujana wangu hasa aliimba nyimbo iliyokwenda kwa jina la siku nzuri ni kijana wa Tanga kama sikosei anaitwa Danny Msimamo katika mashairi yake yenye kibwagizo kisemacho "siku nzuri inavyokwenda wewe mwenyewe utaipenda ×2." na mashairi mengi yaliyotulia ndani yake daaah ilipendeza sana,ndivyo ambavyo mashabiki wa Yanga SC siku ya Jumamosi baada ya ushindi wa ugenini dhidi ya Township Rollers walivyokuwa na furaha na kuona kila kitu kinakwenda sawa na hapo ndipo unapoweza kupata raha katika mchezo wa soka na kufanya uwe ni mchezo unaoshika hisia za watu wengi kutokana na matokeo mbalimbali kuna wakati kwenye soka  1+1  sio lazima jibu liwe 2 kwani jibu linaweza kuwa 3,4 au 5 ndio raha ya mchezo wa soka.
    Yanga wanakila sababu ya kufurahi na kutamba kutokana na presha waliyokuwa nayo baada ya matokeo ya 1-1 wakiwa nyumbani huku wakiwa na mwanzo usio mzuri sana na pengine watu kudhani kule Botswana walienda kukamilisha ratiba tu kitu ambacho kimekuwa tofauti na matarajio ya wengi, watoto wa mjini wanasema wamepindua meza kibabe ni pongezi kwao.
    Sasa wamefanikiwa kuingia hatua ya kwanza ambapo watachuana na timu ya ZESCO united  kutoka nchini Zambia katika mechi ya awali ambayo itachezwa kati ya  tarehe 14/15 mwezi wa 9.
    Katika makala za huko awali nimezungumzia sana ubora na mapungufu ya Yanga kwa kina, leo nijikite kuelekea mchezo ujao dhidi ya Zesco kwani ikumbukwe kuwa kama Yanga sc wanatakiwa kushinda kwa ushindi wa jumla watakuwa wanaingia hatua ya makundi na kujihakikishia kitita zaidi ya Bilioni 1.2 jambo ambalo si dogo ni hatua na mafanikio ya klabu lakini pia kwa manufaa ya mpira wetu,na kama watatolewa na ZESCO basi watacheza mchezo mmoja katika kutafuta nafasi ya makundi katika kombe la shirikisho barani Afrika.

    Nini kifanyike kulekea michezo miwili dhidi ya ZESCO UNITED??

    1.●Matumizi bora ya uwanja wa nyumbani.
    Ukifatilia soka la Afrika kwa ujumla timu nyingi ambazo zimefanikiwa kupiga hatua katika michuano ya kimataifa na hata timu za Taifa ni zile ambazo zinatumia vyema viwanja vyake vya nyumbani kitu ambacho Yanga SC kimekuwa kikiwapa tabu sana,sasa wanatakiwa wabadilike na kuhakikisha wanapata matokeo mazuri nyumbani ili ugenini waende kumalizia kazi tu na hakuna sababu za kushindwa kuwika nyumbani huku wakichagizwa na mashabiki lukuki ambao ni mtaji tosha katika uwanja wa nyumbani,hivyo kuanzia viongozi,wachezaji na mashabiki kila kundi kwa nafasi yake waone namna bora ya kujipanga na kufanikisha ushindi kwani ni hatua muhimu sana kuelekea kwenye kujenga taswira mpya ya klabu yao.
    2.●Benchi la ufundi kuna kazi ya ziada ya kufanya.tokea mechi ya kwanza ya kimataifa ya kujipima nguvu ambapo Yanga SC walipambana na Kariobang Sharks katika uwanja wa Taifa na kupata matokeo ya sare ya 1-1 kumekuwa na makosa ambayo yameendelea kuiweka timu katika wakati mgumu hasa kwenye safu ya ushambuliaji kwani timu imeshindwa kutengeneza nafasi kama timu zaidi ya kutumia uwezo wa mchezaji mmoja mmoja jambo ambalo huwezi litegemea wakati wote ndio mana hadi tunavyozungumza aina ya magoli ambayo timu imekuwa inapata ni kutokana na mipira iliyokufa si jambo baya ila inatakiwa iwe ni chaguo la pili baada ya chaguo la kwanza kushindikana,lakini pia ukitoa safu ya ulinzi pekee maeneo yaliyobaki kwa maana ya eneo la kiungo na ushambuliaji bado hayana muunganiko zaidi ni uchezaji wa kujitoa zaidi kuliko mbinu bora za kimfumo na timu kupata matokeo..
    3.●Kocha ana kazi ya kuangalia upya kikosi cha kwanza.
    Msimu huu Yanga SC wamesajili kikosi kipana ambacho kimesheheni wachezaji wenye vipaji vya hali ya juu huku wengi wakiwa ni vijana ambao bado wapo kwenye nafasi ya kujifunza na kukua zaidi, watu kama Makame,Balama,kalengo,Sibomana,Bigirimana,Ally ally,Ally Mtoni,Metacha na Muharami jambo ambalo ni faida kwa timu ingawa sasa mwalimu anaonekana kuwa kwenye wakati mgumu hasa kwenye namna ya kuwatumia na hii yote ni kutokana na muda mchache aliokaa na timu na kwa sasa timu ipo mashindanoni jambo linaloleta ugumu katika kufanya marekebisho ya msingi,hivyo kwa kutumia mechi za ligi inaweza kuwa fursa kwa mwalimu kuanza kubadili mana ya kikosi kinavyocheza na kuingiza sura mpya kikosini kwani uwezo alio nao kijana Makame,lakini pia mfumo unaotumika hasa sehemu ya kiungo pamekuwa na shida jambo linalopelekea mawinga muda mwingi kutumika kutatua matatizo ya ukabaji sehemu hiyo huku wakipoteza jukumu kubwa la kushambulia na kupunguza kazi za washambuliaji,lakini pia ana hitajika mshambuliaji aliyetimia wa kati na kwa jinsi kikosi kilivyo naona yupo mmoja tu David Molinga ambaye naye ameendelea kupigania kupunguza uzito huku michuano ikiwa imenza jambo linalo hatarisha upatikanaji wa mabao kwani,Balinya ni mshambuliaji namba mbili huku Sadney akiwa mzuri kushambulia kwa kutokea pembeni.
    Kwa upande wa kulia naona bado Juma Abdul anahitajika sana kutokana na msaada wake  mkubwa kwenye kusaidia kupiga krosi zenye macho tofauti na kijana chipukizi Paul Godfrey ambaye sikumbuki lini alipiga krosi iliyozaa bao ingawa ni kijana mzuri kwenye kukaba na kufanya recovery uwanjani ila soka la kisasa kila mchezaji anajukumu la kuanzisha mashambulizi na kuisaidia timu kupata matokeo,Juma Abdul anahitajika kikosini hasa mechi za kimataifa.
    Pia upande wa kushoto ukiacha kazi nzuri ya ukabaji inayofanywa na Ally Mtoni inahitajika mlinzi wa kushoto mwenye kasi na uwezo wa kushambulia huku akikumbuka majukumu yake ya ulinzi pindi timu inapopoteza mpira kwani Ally Mtoni ni mzuri zaidi kucheza kati na Lamine Moro huku nikimuona Kelvin Yondani kwa ukomavu wake na uzoefu akisogezwa kucheza kiungo mkabaji pamoja na Makame au Feisal huku juu yao akikaa Mohamed Issa nadhani utakuwa muunganiko wenye tija,wengi watashangaa kwanini Yondani?ndio ni Yondani kwani kwa muda sasa amekuwa akipandisha mashambulizi na kupiga mipira mirefu yenye macho huku pia akiwa na uwiano mzuri wa kukaba na kushambulia japo anacheza kama namba 4.
    4.●Wakati wa mashabiki kuiamini timu na kuiunga mkono.
    Niliwahi kuwasikia makocha Jose Mourinho,Wenger,na Pep Guadiolla wakikiri kuwa miongoni mwa viwanja vigumu kucheza ni uwanja wa Anfield ambao ndio uwanja wa nyumbani wa Liverpool sio kwa ajili ya uzuri wa uwanja au ukubwa wa kiwanja hapana ila ni zile shangwe zisizokoma muda wote inakuwa ni zaidi ya kelele muda wote wanaanikiza kwa timu yao,wanawatia moyo mashujaa wao bila kujali wanaongoza au wametanguliwa ni mwanzo mwisho ndio mana ni mara chache sana liverpool kupoteza nyumbani,hivyo ifike wakati sasa mashabiki wa Yanga sc mbadilike hakuna Yanga nyingine duniani isipokuwa hii ambayo mmeichagua wenyewe ndio timu yenu hakuna wa kumwachia tambueni wachezaji wanahitaji sana Sapoti yenu niliona wachezaji wa kariobang wakiduwaa ule umati siku ya kilele cha wiki ya mwananchi,swali la kujihoji ule umati umeenda wapi?mnataka nani akawasaidie kushangilia? Mchango wenu kwa wachezaji ni upi au kukaa kwenye luniga na kulaumu?hapana ifike mahali amueni kuzima Television na kwenda uwanjani mkiwa mmevalia jezi zenu huku mkishangilia mwanzo mwisho kwa kuwapa sapoti wachezaji wenu mtakuwa mnawatia moyo lakini pia mnaongeza mapato ya Timu yenu pendwa ambayo mmeichagua wenyewe..
    Mwisho hakuna mafaniko bila mshikamano, wote kwa umoja wenu kila mmoja atimize majumu yake kuhakikisha timu inakuwa na ari na hamasa ya hali ya juu katika michezo miwili ijayo.
    Mkiamua na kushikamana ZESCO mbona mapema tu hawamo.
    (Dominic Salamba ni mchambuzi wa Soka anapatikana pia Instagram kupitia akaunti ya @dominicksalamba au nambari +255713942770)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HONGERA YANGA SC KWA KUITOA ROLLERS, LAKINI ILI KUITOA ZESCO... Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top