• HABARI MPYA

    Thursday, November 01, 2018

    SIMBA SC YAWAFUATA JKT TANZANIA MJINI TANGA BILA BEKI WAKE MGHANA ASANTE KWASI MAJERUHI

    Na Nasra Omary, DAR ES SALAAM
    WAKATI mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Simba wakielekea mjini Tanga kwa ajili ya mchezo wao dhidi ya JKT Tanzania jana, beki mghana Asante Kwasi ameshindwa kusafiri na timu kutokana na majeraha aliyokuwa nayo.
    Kwasi aliumia misuli ya nyama za paja kwenye mchezo wa raundi 11, dhidi ya Alliance, uliochezwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, ambapo simba waliibuka na ushindi wa bao 5-1.
    Simba wanatarajiwa kuwa wenyeji kwenye mchezi wa raundi ya 13, ya Ligi Kuu Tanzania Bara utakaochezwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.

    Asante Kwasi (kushoto) ameshindwa kusafiri na timu kutokana na majeraha aliyokuwa nayo

    Akizungumza na waandishi wa habari kwenye makao makuu ya klabu hiyo, Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara, alisema kuwa kikosi chote kipo fiti isipokuwa Kwasi ambaye bado anaendelea na matibabu.
    Alisema kuwa mwalimu amemuhakikishia kuwa timu imajipanga vizuri na inakwenda kwa ajili ya kujizolea pointi tatu.
    "Kikosi kipo vizuri na wachezaji wote wapo fiti na wanamorari ya kutosha kuelekea mchezo dhidi ya JKT Tanzania japokuwa mchezo utakuwa mgumu na wenye ushindani ila tunaamini lazima turudi na pointi tatu muhimu," alisema Manara.
    Hata hivyo Manara aliweka wazi kuwa beki wako Yusuph Mlipili bado yupo kwenye kikosi cha Simba na yupo pamoja na wezake kuelekea Tanga.
    Lakini pia alisema kuwa licha ya kuwa na kikosi kizuri na kipana wachezaji wao Erasto Nyoni na James Kotei wamerejea kikosi kwa kumaliza adhabu yao ya kutumikia kadi tatu za njano.
    Kwenye msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Simba wapo nafasi ya tatu kwa pointi 23 wakicheza michezo 10 ya Ligi, huku JKT Tanzania wapo nafasi ya tano  wakiwa na pointi 18 wamecheza michezo 11.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC YAWAFUATA JKT TANZANIA MJINI TANGA BILA BEKI WAKE MGHANA ASANTE KWASI MAJERUHI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top