• HABARI MPYA

    Monday, November 19, 2018

    SIMBA SC YAMPELEKA KAPOMBE AFRIKA KUSINI KWA MATIBABU BAADA YA KUUMIA MAZOEZINI AKIWA NA TAIFA STARS

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KLABU ya Simba imempeleka beki wake, Shomari Salum Kapombe mjini Cape Town nchini Afrika Kusini kwa ajili ya vipimo vya maumivu ya kifundi cha mguu.
    Hiyo ni baada ya beki huyo wa kulia anayeweza kucheza kama kiungo pia kuumia enka Jumatano iliyopita katika mazoezi ya timu yake ya taifa, Tanzania hivyo kukosekana jana Taifa Stars ikichapwa 1-0 na wenyeji, Lesotho katik mchezo wa Kundi L kufuzu Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) mwakani nchini Cameroon.
    Kapombe, beki wa zamani wa Azam FC aliyewahi kuchezea AS Cannes ya Ufaransa, aliumia baada ya kuukanyaga mpira vibaya, mguu ukacheza wakati Taifa Stars ikijiandaa na mchezo wa jana katika kambi yake ya siku 10 mjini Bloemfontein, Afrika Kusini.

    Shomari Kapombe (kushoto) akiwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Simba SC, Swedi Nkwabi mchana asubuhi mjini Cape Town

    Jitihada za madakatri wa Taifa Stars, Richard Yomba na Gilbert Kigadya kumponya Kapombe hazikufanikiwa na baada ya mchezo wa jana, leo Mwenyekiti wa Bodi ya klabu ya Simba SC, Swedi Nkwabi amemsafirisha hadi Cape Town kwa vipimo vitakavyofuatiwa na matibabu.
    Kikosi cha Taifa Stars kimerejea Dar es Salaam baada ya kipigo cha jana na sasa kitajipanga kwa mchezo wa mwisho dhidi ya Uganda Machi mwakani kujaribu nafasi ya mwisho ya kufuzu AFCON ya mwakani nchini Cameroon. 
    Baada ya kipigo cha jana kilichotokana na bao la beki wa klabu ya Matlama ya Maseru, Nkau Lerotholi dakika ya 76 kwa kichwa akimalizia mpira wa kona kutoka upande wa kulia, sasa timu yoyote kati ya tatu, Lesotho, Tanzania na Cape Verde inaweza kuungana na vinara wa kundi hilo, Uganda kwenda Cameroon katikati ya mwaka ujao.
    Mamba wa Lesotho wanapanda nafasi ya pili baada ya kufikisha pointi tano sawa na Tanzania, wakati Papa wa Bluu, Cape Verde wanashika mkia kwa pointi zake nne.
    Lesotho ikiifunga Cape Verde Machi mwakani itafuzu AFCON hata kama Tanzania itaifungaje Uganda mjini Dar es Salaam kwa sababu ya matokeo ya mechi zilizohusisha timu zilizofungana kwa pointi.
    Cape Verde nayo itafuzu ikiifunga Lesotho na Tanzania ikalazimishwa sare na Korongo wa Uganda. Taifa Stars inaweza kufuzu iwapo itaifunga The Cranes na Cape Verde ikashinda au kutoa sare na Lesotho katika mechi za mwisho.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC YAMPELEKA KAPOMBE AFRIKA KUSINI KWA MATIBABU BAADA YA KUUMIA MAZOEZINI AKIWA NA TAIFA STARS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top