• HABARI MPYA

    Monday, November 19, 2018

    MESSI NA TAMAA YA FISI MLA MIZOGA HUKU ANATAMANI NYAMA NONO

    Na Socrates Maganga, DAR ES SALAAM
    JARIBU kumfuatilia fisi msituni ana tabia ya kipekee kabisa anamlio wa kwake tu achana na mwendo wake. Wanazuoni waliobobea katika lugha ya kiswahili humuita bwana afya wa porini. Fisi haachi kitu anatafuna kila kilichombele ya macho yake. Mifupa iliyowashinda chui na simba yeye kwake ni nyama laini sana. 
    Lakini sidhani kama Fisi hatamani kabisa kula nyama tamu, siamini kwamba daima anapenda kula mifupa na nyama zilizooza.
    Kila binadamu ana ndoto ya mafanikio katika jambo analolifanyia kazi tena mafanikio haswaa lakini si wote wanaojaaliwa kuyafikia mafanikio hayo wengine ni kwa kupenda wao na wengine ni kwakuangushwa na watu. Moja katika ya watu wanaotamani mafanikio zaidi katika kazi yake ni Lionel Messi mchawi mmoja wa mpira katika viunga vya pale Catalonia huyu jamaa anaijua kazi yake haswa  anaipenda na kila siku anatamani kupata mafanikio zaidi na zaidi.

    Lionel Messi mchawi mmoja wa mpira katika viunga vya pale Catalonia

    Achilia mbali tuzo tano za mwanasoka bora duniani sahau kuhusu pichichi kibao alizojibebea katika historia yake futa kabisa kumbukumbu za mataji anayoyanyajua kila leo pale Nou Camp, hivi vitu vimeshakua vya kawaida sana kwa Messi amevizoea matamanio yake kwasasa ni kunyanyua walau kikombe kimoja tu na timu yake ya taifa ya Argentina walau kimoja tu moyoni kwake nahisi angeambiwa achague kati ya tuzo tano za mwanasoka bora ulimwenguni na kombe moja tu la mataifa America kusini (Copa Libereto) sina shaka Messi angechagua kikombe hicho kimoja.
    Pale nchini Hispania hasa katika jimbo la Catalonia Messi ni Mungu mtu wao wanamuheshimu wanamuamini wanampenda wanatamani hata angekua muhispaniola, Messi ameweza kufuta historia ya Ronaldinho ameweza kuwafanya wanabarcelona kusahau kila mchezaji mzuri aliewahi kupita katika timu yao, kwao Lieonel Messi ni kila kitu kwasababu kawapa kila kitu wanakila sababu ya kujivunia yeye hakuna alichowanyima. Lakini kule nchini Argentina habari ni tofauti watu wanajiuliza uwezo wake katika timu yao ya taifa iliyosheheni mastaa kibao kutoka kila kona ya dunia lakini bado wanashindwa kuinua kwapa kwao wanaamini hakuna mchezaji atakaekuja kuziba pengo la Diego Almando Maradona.
    Maradona kawapa kila kitu wana Argentina alijitoa sana kwaajili yao aliwaweka mabegani mwake pale walipokua katika hali tete kimchezo kitu ambacho kinaonekana kukosekana kwa Messi katika michuano mikubwa, wote tunasahau kuwa Messi ndie aliewapeleka waargentina kule nchini Russia katika fainali za kombe la dunia hakuna anaejali hilo wote tunachotazama ni kwanini Argentina ya Lionel Messi haipati matokeo mazuri katika kombe la dunia. Messi anakua mchungu kwa taifa lake anaumia na kipaji chake leo hii kila Christiano Ronaldo akifunga watu wanarudi kulaumu kwa Messi kwanini hafungi ikiwa Argentina imejaa vipaji lukuki kuliko Ureno. 
    Ni kweli kabisa Argentina ina kila aina ya kipaji katika soka kila nafasi moja uwanjani ina wachezaji wawili zaidi wa kiwango cha dunia lakini hawa jamaa hawajitumi hawana msaada kwa Messi, nani anahesabu magoli ya wazi anayokosa Aguero na mwenzie Higuain nani anahesabu makosa ya golikipa achilia mbali makosa ya mabeki wao lakini lawama zote zinarudi kwa Messi wanasahau kuwa mpira si mchezo wa mtu mmoja bali ni timu nzima. Leo hii Ronaldo anapewa sifa zake kwasababu wenzake uwanjani wanamsapoti akifunga wao wanakaba kweli kweli akikosa wanampigia makofi nao wanajaribu bahati zao lakini kwa Messi habari ni tofauti watu wanataka acheze kila nafasi uwanjani kipa yeye beki yeye kiungo yeye winga yeye mshambuliaji yeye hawa wengine wanafanya kazi gani uwanjani? 
    Kila kosa linalotokea uwanjani basi lazima litakwenda kwa Messi kila timu itakapocheza vibaya basi lawama zitakwenda kwake tunawasahau wengine walioshindwa kutimiza majukumu yao uwanjani. Tunataka Messi acheze Argentina kama anavyocheza Barcelona tunasahau kuwa pale barca kila mtu aliepo uwanjani anatimiza majukumu yake. Kila mchezaji wa soka anatamani mafanikio makubwa na kushinda kila kitu katika maisha yake ya soka lakini si wote wanaofanikiwa.
    Waswahili wanamsemo wao wanasema Mungu hakupi kila kitu na hakunyimi vyote pia Messi amepewa kipaji cha kuogofya lakini amenyimwa wapambanaji kama yeye katika ngazi ya taifa. Messi anatamani sana kushinda kitu na Argentina anaumia sana kukosa mafanikio katika ngazi ya kimataifa hasemi ila moyoni anaumia kumuona hasimu wake mkubwa Ronaldo akibeba ndoo na Ureno anatamani japo Ronaldo  na yeye asingefanya hivyo ili apate kwa kujificha lakini imekua ngumu. Sio kila siku fisi anafurahia mifupa na mizoga hapana anazitamani sana nyama nono, lakini uwezo wa kuzipata hana.
    (Mwandishi wa makala haya, Socrates Maganga na mwanafunzi wa chuo cha Uandishi wa Habari mjini Dar es Salaam, DSJ),
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MESSI NA TAMAA YA FISI MLA MIZOGA HUKU ANATAMANI NYAMA NONO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top