• HABARI MPYA

    Sunday, November 25, 2018

    AKINA SAMATTA WACHAPWA 2-1 NA TIMU YA MDOGO WAKE HAZARD ANAYECHEZA CERCLE BRUGGE KWA MKOPO KUTOKA CHELSEA

    Na Mwandishi Wetu, GENK
    MSHAMBULIAJI  wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta usiku wa jana amecheza kwa dakika zote 90, timu yake, KRC Genk ikipoteza mchezo wa kwanza wa msimu Ligi Daraja la Kwanza A Ubelgiji baada ya kuchapwa 2-1 na Cercle Brugge, tena nyumbani Uwanja wa Luminus Arena mjini Genk.
    Katika mchezo huo, wageni Cercle Brugge walitangulia kwa mabao ya beki Mghana, Joseph Aidoo aliyejifunga dakika ya 26 na mshambuliaji Mtogo, mzaliwa wa Ufaransa Serge Gakpe dakika ya 35, kabla ya mshambuliaji kinda Mbelgiji Leandro Trossard kuifugia la kufutia machozi Genk dakika ya 90 na ushei.
    Kiungo wa mkopo kutoka Chelsea, Kylian Hazard mwenye umri wa miaka 23, anayefuata nyayo za kaka zake wawili, Eden wa The Blues pia na Thorgan wa Borussia Monchengladbach ya Ujerumani, aliingia dakika ya 85 kuchukua nafasi ya Gianni Bruno 85 upande wa Cercle Brugge.
    Mbwana Samatta akimtoka kipa wa Cercle Brugge Paul Nardi jana Uwanja wa Luminus Arena mjini Genk
    Kipa wa Cercle Brugge Paul Nardi akimuingia Mbwana Samatta kuokoa jana 
    Mbwana Samatta akisikitika baada ya kupoteza nafasi nzuri dhidi ya kufunga Cercle Brugge jana

    Pamoja na kupoteza mechi yake ya kwanza msimu huu, Genk inaendelea kuongoza Ligi ya Ubelgiji kwa pointi zake 35 baada ya kucheza michezo 16, ikifuatiwa na Club Brugge yenye pointi 31 za mechi 16, Antwerp pointi 31 mechi 15 na Anderlecht pointi 30 mechi 15.
    Cercle Brugge yenyewe baada ya ushindi wa jana inafikisha pointi 22 katika mechi ya 16 na kujiinua kwa nafasi tatu hadi ya nane kwenye msimamo wa ligi hiyo yenye timu 16.
    Samatta jana amecheza mechi ya 130 katika mashindano yote tangu amejiunga na KRC Genk Januari mwaka 2016 akitokea TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) akiwa jumla ya mabao 51.
    Katika Ligi ya Ubelgiji pekee amefikisha mechi 101 na kufunga mabao 36, Kombe la Ubelgiji mechi nane na mabao mawili na Europa League mechi 21 mabao 14.
    Kikosi cha KRC Genk kilikuwa; Vukovic, Maehle/Gano dk72, Aidoo, Dewaest, Uronen, Berge, Heynen/Malinovskyi dk46, Pozuelo, Ndongala/Paintsil dk55, Trossard na Samatta.
    Cercle Brugge; Nardi, Taravel, Kone, Gakpe/Hazard dk77, Bruno/Palun dk85, Mercier, Cardona/De Belder dk75, Etienne, Lambot, Lusamba na Ueda.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AKINA SAMATTA WACHAPWA 2-1 NA TIMU YA MDOGO WAKE HAZARD ANAYECHEZA CERCLE BRUGGE KWA MKOPO KUTOKA CHELSEA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top