• HABARI MPYA

    Friday, March 10, 2017

    SERENGETI BOYS KUCHEZA NA UGANDA, RWANDA NA BURUNDI UWANJA WA KAITABA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    SHIRIKISHO la Soka Afrika (CAF) likirejesha nyuma kwa wiki moja Fainali za Afrika za vijana chini ya umri wa miaka 17, Tanzania ‘Serengeti Boys’ inatarajiwa kuanza kambi yake Machi 12, mwaka huu mjini Dar es Salaam.
    Serengeti Boys itakuwa kambini Dar es Salaam hadi Machi 26, mwaka huu ambako itakwenda Bukoba mkoani Kagera kwa ajili ya mechi za kirafiki za kimataifa kujiandaa na michuano Afrika ambayo sasa itaanza Mei 14, 2017 badala ya Mei 21, mwaka huu.
    Michezo ya kirafiki ya kimataifa itakuwa ni dhidi ya timu za vijana za Rwanda (Machi 28, 2017), Burundi (Machi 30, mwaka huu) na Uganda Aprili 2, mwaka huu). Michezo yote itafanyika Uwanja wa Kaitaba, Bukoba mkoani Kagera.
    Sababu za kuwa na mechi hizo Bukoba ni kupunguza gharama kwa TFF kwani ni rahisi kusafirisha timu hizo kutoka nchi jirani za Rwanda, Burundi na Uganda.
    Timu hiyo itarejea tena Dar es Salaam Aprili 3, mwaka huu ambako siku inayofuata itaagwa kwa kupewa bendera na mmoja wa viongozi wa nchi kabla ya kusafiri Aprili 5, mwaka huu kwenda Morocco kwa ajili ya kambi.
    Timu hiyo itaunganisha kwenda Cameroon Mei mosi, mwaka huu ambako Mei 3, 2017 itacheza mechi ya kwanza na Cameroon kabla ya kurudiana Mei 6, mwaka huu na siku inayofuata itakwenda Gabon.
    Serengeti Boys ni timu ya vijana ambayo imefuzu kwa fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika zitakazofanyika Gabon kuanzia Mei 14, mwaka huu. Timu hiyo imepangwa Kundi ‘B’ pamoja na mabingwa watetezi Mali, Niger na Angola. Ina lalengo ya kurejea na Kombe la Afrika kwa vijana.
    Ikitokea imekosa nafasi hiyo angalau ikafika nusu fainali ambako kwa mafanikio hayo itakuwa tayari ina tiketi mkononi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia huko India, Novemba, mwaka huu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SERENGETI BOYS KUCHEZA NA UGANDA, RWANDA NA BURUNDI UWANJA WA KAITABA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top