• HABARI MPYA

    Wednesday, October 05, 2016

    SAANYA ‘AENDA NA MAJI’, KADI NYEKUNDU YA MKUDE YAFUTWA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    REFA Martin Saanya aliyechezesha mechi ya watani wa jadi, Simba na Yanga Oktoba 1, mwaka huu amefungiwa miaka miwili kwa pamoja na Msaidizi wake, namba moja, Samuel Mpenzu.
    Habari za ndani kutoka Bodi ya Ligi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), zimesema kwamba maamuzi hayo yamefikiwa leo katika kikao cha Kamati ya Masaa 72 ya shirikisho hilo.
    Na pamoja na kuwafungia waamuzi huo kwa makosa ya kutoa maamuzi ya utata, pia Kamati imefuta Kadi nyekundu ya mchezaji Jonas Mkude baada ya kubaini hakufanya kosa.
    Jonas Mkude (kulia) akizuiwa na wenzake asimfuate refa Martin Saanya (kushoto)
    Maamuzi ya utata ya Saanya yalisababisha vurugu Uwanja wa Taifa Jumamosi baada ya Yanga kupata bao la kuongoza lililofungwa na mshambuliaji Mrundi, Amissi Joselyn Tambwe katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania bara.
    Tambwe alifunga bao hilo dakika ya 26, akimalizia pasi ndefu ya beki Mbuyu Twite na kugeuka mbele ya beki wa Simba, Novat Lufunga kabla ya kufumua shuti lililomshinda kipa Vincent Angban.
    Bao hilo lilizua kizaazaa, wachezaji wa Simba wakimvaa refa Martin Saanya wakidai mfungaji, Tambwe aliushika mpira kabla ya kufunga. Na katika vurugu hizo, Saanya alimtoa kwa kadi nyekundu Nahodha wa Simba SC, Jonas Mkude dakika ya 29 kwa sababu ndiye aliyekuwa mstari wa mbele.
    Kwa hali hiyo, mchezo ukasimama kwa takriban dakika tano baada ya mashabiki wa Simba kuanza kufanya vurugu waking’oa viti na kutupa uwanjani. Polisi walitumia milipuko ya gesi za kutoa machozi kuwatuliza mashabiki hao na mchezo ukaendelea hadi Simba SC wakasawazisha dakika ya 87 kwa bao la Shizza Kichuya.
    Na Mpenzu naye anadaiwa kukataa bao safi la Simba lililofungwa na Ibrahim Hajib mapema kipindi cha kwanza akidai aliotea.
    Pamoja na hayo, Simba na Yanga zote zimeadhibiwa kwa kutozwa faini na kutakiwa kufidia gharama za uharibifu mbalimbali ambao mashabiki wake walifanya uwanjani.
    Taarifa rasmi ya Kikao hicho inatarajiwa kutolewa mapema Jumatano na TFF.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAANYA ‘AENDA NA MAJI’, KADI NYEKUNDU YA MKUDE YAFUTWA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top