• HABARI MPYA

    Thursday, December 05, 2019

    KASEJA, SURE BOY, IDDI NADO NA CHILUNDA WATEMWA KILIMANJARO STARS IKIENDA UGANDA

    Na Saada Akida, DAR ES SALAAM
    KIPA mkongwe, Juma Kaseja wa KMC ni miongoni mwa wachezaji 11 walioenguliwa kwenye kikosi cha Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars kwa ajili ya michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Challenge inayotarajiwa kuanza kesho.     
    Wengine walioenguliwa ni pamoja na nyota watatu wa Azam FC, viungo Salum Abubakari ‘Sure Boy’, Iddi Suleiman ‘Nado’ na mshambulaji Shaaban Idd Chlunda, ngawa sababu haswa za wachezaji hao wa kikosi cha kwanza cha Taifa Stars pia kuachwa hazijatajwa.  
    Wengine walioachwa kutoka kikosi cha awali ni Salum Kimenya wa Tanzania Prisons, Abdulmajid Mangalo wa Biashara United, Fred Tangalu wa Lipuli FC, Kelvin John wa Football House, Jaffary Kibaya wa Mtibwa Sugar, Eliud Ambokile wa TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Yusuph Mhilu wa Kagera Sugar.
    Benchi la ufundi la Kilimanjaro Stars chini ya Juma Mgunda, anayesaidiwa na Suleiman Matola wote wachezaji wa zamani wa timu hiyo limetaja orodha ya mwisho ya wachezaji 22 walioondoka leo kwenda nchini Uganda kwa ajili ya michuano hiyo inayotarajiwa kuanza kesho hadi Desemba 19, mwaka huu.
    Kuna mshambuliaji wa IK Frej Taby ya nchini Sweden Rashid Chambo aliyeongezwa kwenye kikosi hicho ingawa hakutajwa katika kikosi cha awali.
    Kikosi kamili cha Kilimanjaro Stars kinaundwa na makipa;  Metacha Mnata (Yanga SC), Aishi Manula (Simba SC) na David Kisu (Gor Mahia).
    Mabeki; Juma Abdul (Yanga SC), Nickson Kibabage (Difaa Hassan El Jadid/Morocco), Gardiel Michael (Simba SC), Mwaita Gereza (Kagera Sugar), Mohamed Hussein ‘Tshabalala’ (Simba SC), Bakari Mwamnyeto (Coastal Union), Kelvin Yondan (Yanga SC) na Baraka Majogoro (Polisi Tanzania).
    Viungo; ni Jonas Mkude (Simba SC), Zawadi Mauya (Kagera Sugar), Muzamil Yassin (Simba SC) na Hassan Dilunga (Simba SC)
    Washambulaji; no Ditram Nchimbi (Polisi Tanzania), Cleoface Mkandala (Tanzania Prisons), Paul Nonga (Lipuli FC), Miraji Athumani ‘Madenge’ (Simba SC), Eliuter Mpepo (Buldcon/Zambia), Lucas Kikoti (Namungo FC) na Rashid Chambo (IK Frej Taby/Sweden).
    Kili Stars, mabingwa wa 1975, 1994 na 2010 watafungua dimba na ndugu zao, Zanzibar ambao ni washindi wa taji la 1995 mcheoz ambao utafanyika Jumapil, kabla ya kurejea dimbabi Desemba 10 kumenyana na Kenya na kukamilisha mechi zao za Kundi C kwa kumenyana na Djibouti Desemba 12.
    CECAFA Challenge ndiyo michuano mikongwe zaidi ya soka barani Afrika ambayo ilianza mwaka 1926 ikijulikana kama Kombe la Gossage hadi mwaka 1966, ilipobadilishwa na kuwa Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati hadi mwaka 1971 ilipobadilishwa tena na kuwa CECAFA Challenge.
    Uganda ndiyo mabingwa wa kihistoria wa michuano hiyo tangu mwaka 1971, wakiwa wamelitwaa mara 14, wakifuatiwa na Kenya mara saba, Ethiopia mara nne na Tanzania mara tatu.
    Mara ya mwisho Tanzania Bara ilitwaa Kombe hilo mwaka 2010 mjini Dar es Salaam ikiwa chini ya kocha Mdenmark, Jan Borge Poulsen.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KASEJA, SURE BOY, IDDI NADO NA CHILUNDA WATEMWA KILIMANJARO STARS IKIENDA UGANDA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top