• HABARI MPYA

    Friday, December 27, 2019

    YANGA SC YASOGEA ‘ANGA ZAKE’ LIGI KUU BAADA YA KUICHAPA TANZANIA PRISONS 1-0 SAMORA

    Na Mwandishi Wetu, IRINGA
    YANGA SC imepanda hadi nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara baada ya ushindi wa 1-0 dhidi ya Tanzania Prisons ya Mbeya jioni ya leo Uwanja wa Samora mjini Iringa.
    Ushindi huo, unawafanya mabingwa hao mara nyingi zaidi wa Ligi Kuu kufikisha pointi 21 katika mchezo wa 10 – na sasa wanazidiwa pointi tatu na Kagera Sugar inayoshika nafasi ya pili, japo imecheza mechi tatu zaidi, wakati mabingwa watetezi, Simba SC wanaongoza kwa pointi zake 28 za mechi 11. 
    Bao pekee la Yanga SC leo limefungwa na kiungo wa kimataifa wa Rwanda, Patrick Sibomana dakika ya tano tu akimalizia mpira wa kurushwa na kiungo Mzanzibari, Abdulaziz ‘Bui’ Makame kutoka upande wa kulia.


    Sifa zimuendee kipa wa Tanzania Prisons, Jeremiah Kisubi kwa kuokoa michomo kadhaa ya hatari kuizuia Yanga SC kupata mabao zaidi.
    Hata kipa wa Yanga, Metacha Boniphace Mnata naye alizuia majaribio mawili ya hatari mno ya Tanzania Prisons kipindi cha pili. 
    Wachezaji wawili wa Yanga, wote viungo walishindwa kumalizia mchezo baada ya kuumia, kwanza Abdulaziz Makame ambaye nafasi yake ilichukuliwa na Nahodha, Papy Kabamba Tshishimbi kutoka Jamhuri ya Kidemokrsa ya Kongo (DRC) na baadaye Deus Kaseke ambaye nafasi yake ilichukuliwa na Mohamed Issa ‘Banka’ dakika ya 84.
    Tanzania Prisons ilimaliza pungufu baada ya mchezaji wake, Adili Buha kutolewa kwa kadi nyekundu dakika ya 90 na ushei kufuatia kuonyeshwa kadi ya pili ya njano.
    Ikumbukwe Bodi ya Ligi iliuhamishia mchezo huo Uwanja wa Samora mjini Iringa baada ya Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya kuharibika katika eneo la kuchezea kufuatia tamasha la muziki lililofanyika usiku wa Jumatano.
    Kikosi cha Tanzania Prisons kilikuwa; Jeremiah Kisubi, Michael Ismail, Laurian Mpalile, Vedastus Mwithambi, Nurdin Chona, Adili Buha, Ismail Aziz/Cleophace Mkandala dk59, Ezekia Mwashilindi/Jumanne Elfadhil dk46, Samson Mbangula, Jeremiah Juma na Benjamin Asukile/Salum Kimenya dk76.
    Yanga SC; Metacha Mnata, Mustafa Suleiman, Jaffar Mohamed, Lamine Moro, Ally Mtoni, Abdulaziz Makame/Papy Kabamba Tshishmbi dk68, Deus Kaseke/Mohamed Isa Banka dk84, Feisal Salum, David Molinga, Raphael Daudi/Mrisho Ngassa dk46 na Patrick Sibomana.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC YASOGEA ‘ANGA ZAKE’ LIGI KUU BAADA YA KUICHAPA TANZANIA PRISONS 1-0 SAMORA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top