• HABARI MPYA

    Wednesday, December 11, 2019

    ANCELOTTI AFUKUZWA NAPOLI BAADA YA KUWAFUNGA AKINA SAMATTA 4-0 LIGI YA MABINGWA

    Na Mwandishi Wetu, NAPOLI
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta usiku wa jana alicheza kiasi cha saa moja na ushei kabla ya kupumzishwa, timu yake, KRC Genk ikichapwa 4-0 na wenyeji, Napoli katika mchezo wa mwisho wa Kundi E Ligi ya Mabingwa Ulaya Uwanja wa San Paolo mjini Napoli.
    Matokeo yanamaanisha Genk inamaliza mechi zake za hatua ya makundi bila ushindi hata mmoja kufuatia kufungwa mechi tano na kutoa sare moja, hivyo kumaliza mkiani mwa kundi hilo, nyuma ya Salzburg iliyovuna pointi saba, Napoli pointi 12 na mabingwa watetezi, Liverpool walioongoza kwa pointi zao 13.
    Mbwana Samatta usiku wa jana alicheza saa moja na ushei kabla ya kupumzishwa, KRC Genk ikichapwa 4-0 na Napoli

    Katika mchezo wa jana, mabao ya Napoli yalifungwa na Arkadiusz Milik matatu dakika ya tatu, 26 na 38 na baada ya Samatta kumpisha Mbelgiji Theo Bongonda, wenyeji wakapata bao la nne kuputia kwa Dries Mertens dakika ya 74 kwa penalty ya panenka.
    Na saa chache baada ya kocha Carlo Ancelotti kuiwezesha Napoli kutinga hatua ya 16 Bora kwa ushindi huo mnono, akafukuzwa kufuata kikao cha baadaye usiku.
    Jana Samatta  amecheza mechi ya sita ya Ligi ya Mabingwa Ulaya akiwa amefunga mabao matatu – na kwa ujumla amecheza mechi 180 katika katika mashindano yote akiwa amefunga mabao 71 tangu ajiunge na KRC Genk Januari mwaka 2016 akitokea TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
    Katika ligi ya Ubelgiji pekee amecheza mechi 139 akiwa amefunga mabao 54, kwenye Kombe la Ubelgiji amecheza mechi 10, amefunga mabao mawili, katika Super Cup mechi moja, Ligi ya Mabingwa Ulaya mabao matatu, mechi sita.
    Kikosi cha Napoli kilikuwa: Meret, Di Lorenzo, Koulibaly, Manolas, Rui, Callejon/Llorente dk79, Allan, Fabian, Zielinski, Mertens na Milik/Lozano dk78.  
    KRC Genk: Vandevoordt, Maehle, Dewaest, Lucumi, De Norre/Borges dk82, Paintsil, Hrosovsky, Berge, Ito, Samatta/Bongonda dk63 na Onuachu.

    Kocha Carlo Ancelotti amefukuzwa Napoli pamoja na kuiwezesha kutinga hatua ya 16 Bora Ligi ya Mabingwa
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ANCELOTTI AFUKUZWA NAPOLI BAADA YA KUWAFUNGA AKINA SAMATTA 4-0 LIGI YA MABINGWA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top