• HABARI MPYA

    Sunday, March 31, 2019

    BOCCO APIGA MBILI, KAGERE MOJA SIMBA SC YAIPIGA MBAO FC 3-0 LIGI KUU MOROGORO

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    SIMBA SC imeendeleza furaha kwa mashabiki wake baada ya ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Mbao FC kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.
    Ushindi huo uliotokana na mabao mawili ya Nahodha John Raphael Bocco na Mnyarwanda Meddie Kagere unaifanya Simba SC ifikishe pointi 57 baada ya kucheza mechi 22, lakini inabaki nafasi ya tatu nyuma ya Azam FC yenye pointi 59 na Yanga SC pointi 67 baada ya wote kucheza mechi 28.
    Bocco, mmoja wa wachezaji waliokuwemo kwenye kikosi cha Tanzania kilichokata tiketi ya Fainali za Kombe la Mataifa uya Afrika mwaka huu nchini Misri wiki iliyopita, alifunga bao la kwanza kwa kichwa  dakika ya 25 akimalizia krosi ya beki wa kushoto Mohammed Hussein ‘Tshabalala’.

    Bao hilo lilidumu hadi mapumziko na kipindi cha pili Bocco akafunga bao la pili kwa penalti dakika ya 59 baada ya beki Peter Mwangosi kuanguka na kuunawa mpira uliopigwa na kiungo Muzamil Yassin.
    Kagere, mwenye asili ya Uganda na kinara wa mabao wa Simba SC msimu huu, akafunga bao la tatu kwa penalti pia dakika ya 79 baada ya yeye mwenyewe kuangushwa na Hamimu Abdulkarim wa Mbao FC.
    Kipa Deogratius Munishi ‘Dida’ aliyeanza badala ya majeruhi Aishi Manula alidaka kwa ustadi mkubwa na kumaliza dakika 90 bila kuruhusu hata bao la kuotea.  
    Kikosi cha Simba SC kilikuwa; Deogratius Munishi ‘Dida’, Zana Coulibaly, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Erasto Nyoni, Pascal Wawa, James Kotei, Haruna Nioyonzima, Muzamil Yassin, John Bocco/Said Ndemla dk73, Meddie Kagere/Adam Salamba dk86 na Mohamed ‘Mo’ Ibrahim/Hassan Dilunga dk61.
    Mbao FC; Metacha Mnata, Erick Murilo, Amos Charles, David Mwassa, Peter Mwangosi, Said Said, Ally Mussa, Herbert Lukindo/Robert Ndaki dk63, Ibrahim Njohole/Zamfuko Elias dk75, Hamim Abdulkarim na Pastory Athanas.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BOCCO APIGA MBILI, KAGERE MOJA SIMBA SC YAIPIGA MBAO FC 3-0 LIGI KUU MOROGORO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top