• HABARI MPYA

    Wednesday, November 01, 2017

    TFF YAZIPA FEDHA TIMU ZOTE ZINAZOSHIRIKI KOMBE LA AZAM

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    WAKATI michuano ya Azam Sports Federation Cup (ASFC), inatarajiwa kuanza kesho, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), tayari limezilipa timu zote sita zinazoanza kuchuana hatua ya awali.
    Mchezo kati ya Kisarawe United ya Pwani na Silabu ya Mtwara umeahirishwa hadi hapo baadaye utakapotangazwa tena kwa sababu ya majeruhi ya wachezaji.
    Baadhi ya wachezaji wa Silabu – mabingwa wa Mkoa wa Mtwara wameumia kutokana na ajali ya gari iliyotokea maeneo ya Mchinga mkoani Lindi wakiwa safarini kwenda Pwani.
    Mechi zinazotarajiwa kufanyika kesho ni kati ya Buseresere ya Geita itayocheza na Isako ya Songwe; ilihali Usamala ya Simiyu itacheza na Sahale All Stars ya Tanga katika mechi hizo za awali kuwania taji la ASFC.
    Ratiba ya Azam Sports Federation Cup 2017
    Baada ya mechi hizo, itakuja Raundi ya Kwanza ya ASFC ambayo itachezwa kati ya Novemba 7, 8 au 9 ambako TFF imepanga kesho Novemba 2, mwaka huu kutuma fedha zote za maandalizi ya timu husika ili kusiwe na kisingizio chochote cha kujiandaa.
    Kaimu Katibu Mkuu wa TFF, Kidao Wilfred ameagiza Idara ya Fedha na Utawala ya TFF kulipa fedha hizo haraka, lakini kwa masharti ya taratibu za malipo kwamba lazima yapitie benki, badala ya akaunti ya mwakilishi ye yote au kiongozi.
    Kidao ameagiza kwamba kwa timu ambayo haijafungua akaunti watakuta fedha hizo kwenye Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa (FA), lakini TFF ingependa kusisitiza kwa wadau hao kufufua akaunti au kufungua akaunti haraka.
    Katika raundi hiyo ya kwanza Mashujaa ya Kigoma itacheza na Mshindi kati ya Buseresere ya Geita na Isako ya Songwe; wakati mechi nyingine zitakuwa Msange ya Tabora itacheza na Milambo pia ya Tabora ilihali Bulyanhulu ya Shinyanga itacheza na Area C ya Dodoma.
    Kwa mujibu wa droo, Mji Mkuu FC ya Dodoma imeangukia kwa Nyundo ya Kigoma wakati Baruti FC ya Mara itacheza na Ambassodor ya Kahama, Shinyanga huku Eleven Stars ya Kagera ikipangwa kucheza na Ndovu ya Mwanza.
    Changanyikeni ya Dar es Salaam itacheza na Reha FC pia ya Dar es Salaam wakati Mshindi kati ya Kisarawe United na Silabu ya Mtwara atacheza na Kariakoo ya Lindi huku Cosmopolitan ikicheza na Ajabalo wakati Makumba FC itapambana na Green Warriors ya Kinondoni wakati Namungo FC ya Lindi itachuana na Villa Squad ya Dar es Salaam huku Dar City ikicheza na Majimaji Rangers ua Nachingwea.
    Michezo mingine ya hatua ya kwanza itakutanisha timu za Shupavu FC ya Morogoro na Sabasaba pia ya mjini humo wakati Motochini FC ya Katavi dhidi ya Ihefu FC ya Mbeya wakati The Mighty Elephant ya itacheza na Makanyagio ya Rukwa.
    Timu ya Burkina FC ya Morogoro itacheza na Mbinga United ya Ruvuma wakati Makambako Heroes ya Njombe  itacheza na Mkamba Rangers ya Morogoro wakati Real Moja Moja itapambana na African Wonderers – zote za Iringa. Boma FC ya Mbeya itacheza na African Sports ya Tanga.
    Mechi nyingine za hatua hiyo itakuwa ni kati ya Pepsi ya Arusha ambayo itacheza na Kilimanjaro Heroes ya Kilimanjaro; huku Stand Misuna ya Singida itacheza na Madini FC ya Arusha ilihali AFC ya Arusha itacheza na Nyanza ya Manyara wakati New Generation itacheza na Mshindi kati ya Usamala FC na Sahale ya Tanga. Bodaboda FC itacheza na Kitayose ya Kilimanjaro.
    Michuano hiyo ambayo Bingwa Mtetezi ni Simba SC ya Dar es Salaam, inashirikisha timu 91 msimu huu kwa mchanganuo wa timu 16 za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL); 24 za Ligi Daraja la Kwanza (FDL); 24 za Ligi Daraja la Pili (SDL) na 27 za Ligi ya Mabingwa wa Mkoa (RCL).
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TFF YAZIPA FEDHA TIMU ZOTE ZINAZOSHIRIKI KOMBE LA AZAM Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top