• HABARI MPYA

    Tuesday, November 07, 2017

    SAMATTA NJE WIKI SITA…MAUMIVU YAKE YANAHITAJI ‘KISU’

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta anatakiwa kuwa nje kwa zaidi ya wiki sita kufuatia kuumia goti Jumamosi akiichezea klabu yake, KRC ikilazimishwa sare ya 0-0 Jumamosi na Lokeren katika mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza A Ubelgiji Uwanja wa Luminus Arena mjini Genk.
    Akizungumza na Bin Zubeiry Sports – Online mchana huu kwa simu kutoka Genk, Samatta amesema kwamba baada ya kufanyiwa vipimo imegundulika mishipa midogo ya kwenye goti lake la mguu wa kulia imechanika, hivyo atahitaji kufanyiwa upasuaji mdogo ili apone sawia.
    “Kuchanika kwa mishipa midogo ya goti, hivyo itachukua wiki sita au zaidi ili kupona, halafu kuna mshipa mwingine (meniscus) umepata tatizo, inatakiwa kufanyiwa upasuaji ndogo kuuweka katika hali nzuri ili isije kusumbua baadaye, hivyo kipindi cha kukaa nje ni wiki sita au zadi,” amesema.
    Samatta sasa hataweza kujiunga na kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars kwa ajili ya mchezo dhidi ya Benin Novemba 11, mwaka huu.
    Samatta alidumu uwanjani kwa dakika 40 Jumamosi tu kabla ya kuumia na kumpisha Nikolaos Karelis aliyekuwa anacheza kwa mara ya pili tangu arejee uwanjani baada ya kuwa nje kwa muda mrefu kutokana na kuwa majeruhi.
    Baada ya kucheza nyumbani mfululizo mechi za kirafiki za kimataifa, Taifa Stars itatoka mwezi huu kwenda Benin kucheza na wenyeji Novemba 11, mwaka huu na kikosi cha wachezaji 24 kilichoingia kambini jana mjini Dar es Salaam, kitaondoka Alhamisi kwenda Benin tayari kwa mchezo huo.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA NJE WIKI SITA…MAUMIVU YAKE YANAHITAJI ‘KISU’ Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top