• HABARI MPYA

    Tuesday, November 01, 2016

    WAJUMBE TFF WAMWAGIA PONGEZI MALINZI 'SHAVU LA CAF'

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    WADAU mbalimbali wakiwamo Wajumbe wa Kamati ya Utendaji wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania, wamemwagia sifa na pongezi Rais wa TFF Jamal Malinzi kwa kuteuliwa kwake kuunda jopo la watu 11 tu wa Kamati maalumu ya mageuzi ya muundo wa CAF itakayokuwa na jukumu la kufanya mabadiliko mapya ya shirikisho.
    Rais wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF), Issa Hayatou amemteua Rais Malinzi ikiwa ni sehemu ya maazimio ya mkutano uliopita wa kawaida wa shirikisho uliofanyika Septemba 29, mwaka huu ambako Rais Hayatou amezingatia mjadala uliolenga kufanya mabadiliko kwa kufanyia kazi mara moja.
    Kamati inaundwa na: Issa Hayatou (Cameroon), ambaye ni Rais CAF atakayekuwa Mwenyekiti, Amadou Diakite (Mali), Makamu Rais wa CAF na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya shirikisho naMohammed Raouraoua (Algeria), Mjumbe wa Kamati ya Utendaji CAF ambaye pia ni Mwenyekiti wa Masuala ya Sheria. Pia ni Rais wa Shirikisho la Soka Algeria (FAF).
    Wengine ni Lydia Nsekera (Burundi) Mjumbe wa Baraza la Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), Raymond Hack (Afrika Kusini), Mwenyekiti wa Bodi ya Nidhamu ya CAF, Prosper Abega (Cameroon), Mwenyekiti wa Bodi ya Rufaa ya CAF, Malinzi (Tanzania), Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Augustin Senghor (Senegal), Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Senegal (FSF).

    Wamo pia Victor Adolfo Osorio (Cap Verde), Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Cap Verde (FCF), Maclean Letshwti (Botswana), Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Botswana (BFA) na Hicham El Amrani (Morocco) ambaye ni Katibu Mkuu wa CAF.
    Baada ya kutangazwa, salamu za wajumbe wa Kamati ya Utendaji zilikuwa ni kama ifuatavyo.
    Lina Kessy, ameandika: “Kwanza Napenda kumpongeza Rais kwa uteuzi huo. Tuna imani naye na tunaamini itaiwakilisha vyema nchi yetu. Huu ni ushahidi tosha wa uwezo wa Rais wetu latika maswala ya utawala. Nakutakia majukumu mema naomba nikungate sikio. Nafasi ya Vice (Makamu) MOJA KATI YA WALE WAWILI IENDE KWA MWANA MAMA... Mwamba ngozi...Nakutakia kila la kheri Rais.  Naamini tutakuwa tayari kukuwezesha kufanikisha majukumu yako. Asante.
    Ayoub Nyenzi, ameandika: “Hongera sana Rais Jamal Malinzi kwa uteuzi huu .Ni jitihada zako za kuendeleza mchezo wa mpira kumesababisha uteuzi huu Mungu akuongoze katika jukumu hilo lililo nje ya mipaka ya Tanzania.
    Blassy Kiondo, naye ameandika: “Napenda kuchukua fursa hii kukupongeza wewe binafsi Mh. Rais kwa Kuteuliwa katika Kamati hiyo muhimu ya Mabadiliko ya Muundo wa Shirikisho la soka la Afrika, CAF.  Uadilifu wako, Juhudi katika Utendaji wako na Uweledi wako busara na hekima ulizonazo ndizo zimepelekea wewe Kuteuliwa kuwa Mjumbe katika Kamati hiyo Hongera sana  Mh. Rais, Hii pia ni sifa kubwa kwa Nchi yetu ya Tanzania, Hongera Jamal Malinzi.
    Salum Chama: “Mimi binafsi nimepata faraja kubwa sana kwa uteuzi alioupata Mh. Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania nampongeza sana kwa kuteuliwa kwake uteuzi huu ni imani kubwa kwa Watanzania na ni kipimo kuwa Rais wetu anatambulika na kioo kwa mataifa ya nje hivyo basi jukumu letu sote nikumuombea kwa allah amjaalie katika majukumu yake mapya, na Mungu akupe afya njema daima.
    Kalilo Samson Mswaga: Nampongeza Mh. Rais wetu kwa kuteuliwa katika nafasi hiyo, Mola azidi kumpa busara aweze kuitangaza zaidi TFF na Tanzania kwa umahiri.
    Alhaji Ahmed Mgoyi: “Rais kwa kweli nimefarijika sana kwa nafasi uliyoaminiwa na kiroho safi nakuahidi pamoja na shughuli nyingi nilizonazo lakini kwa uzito wa jambo hili nimejitolea kuwa nakusindikiza katika shughuli zako ngumu za Kamati hii. President Hongera sana. Inshaalla, Tupo Pamoja. Kila la Kheri,".
    Kamati hiyo itawajibika kwa Kamati ya Utendaji ya CAF ili kupata mwongozo ingawa haibanwi zaidi na Katiba ya shirikisho.
    Malinzi (kushoto) akiwa na Rais wa CAF, Issa Hayatou (kulia)

    Kamati hiyo imeundwa ikiwa ni sehemu ya maazimio ya mkutano uliopita wa kawaida wa CAF uliofanyika Septemba 29, mwaka huu ambako Rais Hayatou amezingatia mjadala uliolenga kufanya mabadiliko CAF kwa kufanyia kazi mara moja.

    Hayatou si tu kwamba amejali mjadala wa mkutano ule, pia ameheshimu mawazo ya vyama wanachama vya nchi pamoja na wajumbe wa Kamati ya Utendaji na wataalamu mbalimbali ili kupata mustakabali wa muundo wa uongozi wa shirikisho hilo ili kukabiliana na changamoto dhidi ya mpira wa miguu barani Afrika.
    Akizungumzia uteuzi huo, Malinzi kwanza alimshukuru Hayatou kwa uteuzi huo ambao umeonyesha moja kwa moja kuwa na imani naye katika kuleta maendeleo ya mpira wa miguu katika muundo mpya.
    “Lakini sifa hii ya kuteuliwa ni yangu pekee kwani ni heshima kubwa ambayo imepewa nchi yetu pendwa ya Tanzania, kadhalika nchi zote za Afrika Mashariki na Kati,” alisema Malinzi alipozungumza.
    Kamati hiyo itawajibika kwa Kamati ya Utendaji ya CAF ili kupata mwongozo ingawa haibanwi zaidi na Katiba ya shirikisho.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: WAJUMBE TFF WAMWAGIA PONGEZI MALINZI 'SHAVU LA CAF' Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top