• HABARI MPYA

    Wednesday, November 23, 2016

    MALINZI AWAPA POLE YANGA KWA MSIBA WA PILI NDANI YA WIKI MOJA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    RAIS wa  Shirikisho la Soka Tanzania  (TFF), Jamal Malinzi amewapa pole mabingwa wa nchi, Yanga SC kufuatia msiba wa pili ndani ya wiki moja, baada ya kifo cha aliyewahi kuwa Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya klabu, miaka ya 1990, Hamad Kiluvia.
    Hamad Kilivua amefariki dunia leo alfajiri Novemba 23, 2016 jijini Dar es Salaam ikiwa ni siku ambayo Makamu Mwenyekiti wa zamani wa klabu hiyo, Isaac Shekiondo ‘Clinton’ amezikwa kwao Korogwe mkoani Tanga.
    Malinzi amesema kifo cha Kiluvia kinaongeza majonzi kwa wana Yanga, kwani kinakuja wakati bado machozi ya kumlilia Shekiondo aliyefariki dunia Novemba 20, mwaka huu kwenye Hospitali ya Amana, Ilala  jijini Dar es Salaam hayajaisha.
    Enzi za uhai wake, Kiluvia pia aliwai kuwa Mjumbe wa Bodi ya Seneti ya klabu hiyo pamoja na Malinzi, aliyekuwa pia Katibu Mkuu wa timu hiyo ya Jangwani.
    Kadhalika Rais Malinzi alituma salamu hizo kwa familia ya marehemu Kiluvia ndugu, jamaa na marafiki ambayo kwa muda walikuwa wakimuuguza mpendwa wao na hivyo kutokana na kifo hicho, amewataka kuwa watulivu kipindi hiki kigumu cha maombolezo ya mpendwa wao.
    Msiba wa Kiluvia uko nyumbani kwake, Mikocheni Regent Estate jirani na Ofisi za Baraza la Mazingira (NEMC) ambako taratibu za mazishi zinafanyika. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MALINZI AWAPA POLE YANGA KWA MSIBA WA PILI NDANI YA WIKI MOJA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top