• HABARI MPYA

    Wednesday, July 29, 2020

    BENJAMIN WILLIAM MKAPA NAJUA UMEENDA, ILA ACHA NISEME!

    Na Dominick Salamba, DAR ES SALAAM
    Dunia ni mahali ambapo tunaletwa ili tuishi.Maisha yetu yananzia kwa wazazi wetu na walezi wetu na kisha tunahamia kwenye jamaa na jamii zetu.
    Huko ndipo hukutana na mengi hukutana na wengine na ndipo urafiki na uadui pia hupatikana,ndipo tunaifahamu Dunia kwa uzuri na ubaya wake.
    Nilikukuta huku kwa jamii nilikuona na kujifunza mengi kupitia kwako nilipata majibu ya maswali yangu hata kabla ya kukuuliza kwani kila ulilosema juu ya maisha na wanadamu lilikuwa linajibu moja ya maswali yangu ya muda mrefu.

    Kuna wakati sio tu pesa na mali zinaweza kukufanya upate amani ya akili,mwili na roho bali hata maneno yenye busara na tumaini yanaweza kukupeleka mbali katika tumaini na tulizo la moyo.
    Leo umeondoka nikiwa bado kijana lakini wewe katika umri wako wa uzee umri ambao hata kibiblia ni zawadi pia kwa maana umeenda katika ile ziada ni jambo la bahati na jema ila bado hainifanyi nisiumie na kuhuzunika juu yako baba.
    Yapo mengi ulisema na kuyaandika mengine tuliyasikia na kuyazingatia ila mengine tuliyaona ya kawaida ila leo kumbe yale tuliyaona ya kawaida ni mazito na ya msingi kuliko tulivyodhani.
    Wewe ni shujaa sio tu wa  fikra zangu bali kwa Dunia msimamo na bidii uliyoifanya katika kulipigania Taifa letu ni alama tosha ya uzalendo na upendo ulionao juu ya Watanzania wote.
    Leo kila kona tunasikia sifa zako sio sifa tu bali ni sifa zinazoendana na vitendo vinavyoonekana kwa macho ulikuwa ni zaidi ya zawadi kwetu,umetukomboa vijana wengi katika utumwa wa fikra,ulipanda mbegu ya uthubutu,ukweli,uwajibikaji na uwazi katika katika fikra zetu leo tunatembea kifua mbele Baba ahsante.
    Mipango yako juu ya ustawi wa Taifa hili ni nani atabeza? msimamo na uongozi wa kusimamia haki na umoja wa Taifa ni nani atapuuza Asante Baba wewe ni mshindi kwetu.
    Tunalia na kuomboleza kwakuwa ni mazoea ya binadamu hasa anapopoteza mpendwa wake ila  kiukweli umeondoka ukiwa umetimiza kwelikweli kufanya katika zamu yako.
    Ahsante baba Taifa litakukumbuka Daima,na umetuachia kiongozi shupavu ambaye ni mbeba maono yako na kweli ameanza kulithibitisha hilo hata kabla haujalala katika nyumba yako ya milele,Asante kwa kutuachia Dr.John Pombe Joseph Magufuli kwani kila tukilia na kuona tumepoteza Baba tunakumbuka kuwa umetuachia Jemedari ambaye anakiongoza chombo sawiya,ahsante baba.
    Mwisho niwaombe watanzania wenzangu tuzidi kushikamana na kudumisha amani umoja na mshikamano tulioachiwa na wazee wetu. Ahsante.0

    (Dominick Salamba ni mchambuzi wa soka,siasa na maswala ya kijamii anapatikana kwa namba +255 713 942 770 na kupitia katika Instagram @dominicksalamba na Twitter @dominicksalamb1)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BENJAMIN WILLIAM MKAPA NAJUA UMEENDA, ILA ACHA NISEME! Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top