• HABARI MPYA

    Saturday, November 10, 2018

    ESPERANCE WABEBA TAJI LA LIGI YA MABINGWA AFRIKA

    TIMU ya Esperance ya Tunisia imetwaa taji la Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Al Ahly ya Misri katika mchezo wa marudiano wa Fainali usiku wa jana Uwanja wa Olimpiki, Rades mjini Tunis, Tunisia.
    Kwa matokeo hayo, Esperance wanabeba taji hilo kwa ushindi wa jumla wa 4-3, kufuatia kufungwa 3-1 kwenye mchezo wa kwanza Ijumaa ya wiki iliyopita Uwanja wa Borg El Arab mjini Alexandria. 
    Pongezi kwake Saad Beguir aliyefunga mabao mawili dakika za 45 na 54 kwa Watunisia hao, kabla ya Anice Badri kufunga la tatu dakika ya 86 na kuwazima wapinzani wao wa Kaskazini mwa Afrika.

    Kwa ushindi huo, Esperance watapatiwa dola za Kimarekani Milioni 2.5, wakati Ah Ahly wanapata dola Milioni 1.25.
    Hilo linakuwa taji la tatu la michuano hiyo kwa Esperance, baada ya awali kulibeba katika miaka ya 1994 na 2011.
    Al Ahly wanabaki kuwa mabingwa mara nane wa kihistoria wa taji hilo, baada ya kushinda katika miaka ya 1982, 1987, 2001, 2005, 2006, 2008, 2012 na 2013.
    Wanafuatiwa na mahasimu wao wa jadi wa Misri,  Zamalek waliochukua taji hilo mara tano katika miaka ya 1984, 1986, 1993, 1996 na 2002 sawa na TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) iliyolibeba taji hilo mara tano katika miaka ya 1967, 1968, 2009, 2010 na 2015. 
    Kikosi cha Esperance jana kilikuwa: Cherifia; Belaili/Meskini dk80, Chemmam, Coulibaly, Derbali, Chaalali, Ben Mohamed, Khenissi/Mejri dk70, Yakoubi, Badri na Beguir/Erbeia dk62.
    Al Ahly: El Shenawy; El Demerdash/Nedved dk62, Samir, Coulibaly, Ashraf, Ashour, El Sulya/El Gaber dk76, Gaber/S.Mohsen dk62, Soliman, Mohareb na M.Mohsen.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ESPERANCE WABEBA TAJI LA LIGI YA MABINGWA AFRIKA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top